logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Gidi amuomboleza kwa hisia marehemu Leonard Mambo Mbotela, afichua alivyochochea kazi yake ya utangazaji

Gidi alifichua jinsi nguli huyo wa redio alivyokuwa akimpigia simu mara kwa mara ili kumtia moyo na hata kumrekebisha pale anapokosea.

image
na Samuel Mainajournalist

Mahojiano07 February 2025 - 12:55

Muhtasari


  • Gidi amezungumzia jinsi marehemu alivyochochea kazi yake na akabainisha kuwa amehuzunishwa sana na habari za kifo chake.
  • Gidi alichukua fursa kumuomboleza marehemu Mbotela na kuwafariji familia, marafiki na mashabiki wake.

Marehemu Leonard Mambo Mbotela na mtangazaji Gidi Ogidi

Mtangazaji wa kipindi cha Gidi na Ghost asubuhi katika Radio Jambo Gidi Ogidi amemuomboleza kihisia mwanahabari mkongwe Leonard Mambo Mbotela.

Habari za kusikitisha za kifo cha mtangazaji huyo wa zamani wa redio zilisambaa kama moto wa nyikani Ijumaa asubuhi, na kuvunja mioyo ya wengi waliomfahamu.

Huku akimuomboleza, Gidi alizungumzia jinsi marehemu alivyochochea kazi yake ya utangazaji na akabainisha kuwa amehuzunishwa sana na habari za kifo chake.

“Nimesikitishwa sana kuskia hiyo habari kuhusu kifo cha mwenda zake,” Gidi alisema kwenye mahojiano ya simu.

“Huyu ni ndugu ambaye tumemfahamu sana, huyu ni ndugu ambaye nimelelewa nikimskiza kwenye redio. Ata mimi kuanza kazi yangu ya redio ni yeye alinivutia. Na miongoni mwa watu ambao nilikuwa najaribu sana kuiga kazi ambayo inafanana na yao kwenye redio ni Mzee Leonard Mambo Mbotela,” alisema zaidi.

Mtangazaji huyo mahiri wa kipindi cha asubuhi alizungumzia athari kubwa ya Leonard Mambo Mbotela katika tasnia ya habari nchini Kenya.

Pia alifichua jinsi nguli huyo maarufu kwa kipindi chake cha ‘Je, huu ni ungwana’ alivyokuwa akimpigia simu mara kwa mara ili kumtia moyo na hata kumrekebisha pale anapokosea.

“Ni huzuni sana kumpoteza gwiji wa redio hapa nchini Kenya. Ni mtu ambaye alikuwa na historia nyingi kuhusu utangazaji hapa nchini Kenya. Mara kwa mara alikuwa ananipigia simu. Ni mtu ambaye ata katika uzee wake alikuwa akinipigia simu ananiuliza tunaendeleaje, ananirekebisha, ananiambia leo niliskia ulisema hivi na kuwa hivi. Alikuwa anafurahia sana, kwa hivyo ni huzuni sana kumpoteza mzee Leonard Mambo Mbotela,” alisema.

Gidi alichukua fursa kumuomboleza marehemu Mbotela na kuwafariji familia, marafiki na mashabiki wake ambao wameguswa sana na taarifa hizo za kusikitisha.

“Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Tunaiombea familia yake, tunawaombea mashabiki wake, na kila mmoja ambaye alikuwa anamfahamu pale” alisema.

Mwanahabari mkongwe wa Kenya Leonard Mambo Mbotela alifariki dunia Ijumaa asubuhi.

Mkwe wake Anne Mbotela alithibitisha habari hizo za kusikitisha kwa Radio Jambo kupitia simu.

Mwanahabari huyo mkongwe alikuwa hajisikii vizuri kwa muda na alikata roho mwendo wa saa tatu unusu asubuhi siku ya Ijumaa.

"Ni kweli baba mkwe wangu amefariki," Anne alisema.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved