logo

NOW ON AIR

Listen in Live

"Kijana wangu alienda mawindoni Uganda!” Ghost Mulee afichua maelezo yasiyojulikana kuhusu mkwe wake mpya

Ghost amefunguka kuhusu harusi ya hivi majuzi ya mwanawe na maelezo ya kipekee kuhusu binti mrembo aliyeoa.

image
na Samuel Mainajournalist

Mahojiano28 February 2025 - 15:13

Muhtasari


  • Katika mahojiano ya kipekee, Ghost alifichua mambo ambayo hayakuwa yamejulikana na Wakenya wengi kuhusu mkwe wake mpya.
  • Ghost alifichua kuwa Jesse alikutana na mke wake wakati akisoma Uganda, na wamekuwa kwenye mahusiano kwa miaka kadhaa.

Mtangazaji wa kipindi cha Gidi na Ghost Asubuhi kwenye Radio Jambo, Jacob ‘Ghost’ Mulee amefunguka kuhusu harusi ya hivi majuzi ya mwanawe Jesse Mutua na maelezo ya kipekee kuhusu binti mrembo aliyemwoa.

Katika mahojiano ya kina na mtayarishaji wa maudhui, Samuel Maina, Ghost alifichua mambo ambayo hayakuwa yamejulikana na Wakenya wengi kuhusu mkwe wake mpya.

Ghost alieleza kuwa mkwe wake anatoka Mbalala, Uganda, kwa jamii ya Waankole.

“Kijana naye alienda mawindoni mpaka Uganda. Tulienda mpaka mji wa Mbalala kwa mahari, maana huyu mwanadada anatoka sehemu fulani ya huko. Ametoka kwa jamii ya Waankole,” Ghost alisema.

Mtangazaji huyo mcheshi alibainisha kuwa Jesse alikutana na mke wake wakati akisoma Uganda, na wamekuwa kwenye mahusiano kwa miaka kadhaa kabla ya kufunga ndoa wikendi iliyopita.

Hata hivyo, wawili hao walikuwa wakiishi tofauti kwani mamake Jesse, mke wa Ghost, alisisitiza kila kitu kifanyike kwa utaratibu unaostahili.

“Mpenzi wake ni mtu ambaye alikutana naye wakati akisoma kule Uganda. Walikutana kama wanafunzi miaka mingi iliyopita, na akaja akasomea hapa USIU. Wamekuwa wapenzi, lakini hawakuanza kuishi pamoja. Mamake, ambaye ni mke wangu, hapendi mambo ya mkato. Yeye anataka kila kitu kifanyike kwa mpangilio. Alimwambia kijana hawezi kuishi na msichana wa mtu kama wazazi wake hawajui,” alisema.

Ghost alizungumzia jinsi alivyokutana na babake binti huyo hapa Kenya kabla ya mipango ya harusi kuanza miaka miwili iliyopita.

“Babake (msichana) ni mtu wa kimataifa. Wakati alipokuja Kenya, tulipata fursa ya kushiriki chakula cha jioni pamoja na tukamwambia kwamba binti yake hajapotea Nairobi. Baada ya utambulisho huo, mipango ilianza rasmi. Tukaenda kufanya mambo ya mahari na taratibu zote, tukamaliza. Imekuwa safari ndefu ya takriban miaka miwili tukipanga harusi hii,” alisema.

Kocha huyo wa zamani wa Harambee Stars pia alifunguka kuhusu mila za wakwe wao na jinsi walivyorahisishiwa baadhi ya taratibu wakati wa maandalizi ya harusi.

“Wana taratibu na mila nyingi sana lakini nashukuru walitupunguzia. Kulingana na mila ya Waankole, tulihitajika kwenda Uganda mara saba kabla ya ndoa. Lakini kwa huruma yao, walipunguza na tulihitajika kwenda mara moja pekee kabla ya wao kuja Nairobi kwa harusi,” alisema.

 Jesse Mutua ni mtoto wa kwanza wa Ghost na ndiye wa kwanza kati ya ndugu zake kufunga ndoa. Alifunga pingu za maisha na mpenzi wake wa muda mrefu katika harusi ya kuvutia iliyofanyika Nairobi wikendi iliyopita.

Ghost alisema kuwa lilikuwa jambo la kujivunia sana kwake kuona mwanawe akifunga ndoa, baada ya kumlea tangu akiwa mtoto mdogo.

“Nilipokuwa kanisani, walipofunganishwa pale, nilijihisi kama kutoa machozi. Si kawaida yangu kulia lakini nilitoa machozi ya furaha nikikumbuka safari ya maisha ya kijana wangu tangu kuzaliwa kwake hadi sasa anapofunga ndoa,” alisema.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved