logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Nimekuwa mvutaji sigara maisha yangu yote lakini sasa nimeacha – Jose Chameleone

“Kabla niondoke kwenye USA nilikuwa nimepoteza takribani kilo 13. Na madaktari hawakunishauri nisifanye chochote, lakini nilitumia tathmini ya Kibinafsi.”

image
na MOSES SAGWEjournalist

Burudani22 April 2025 - 09:42

Muhtasari


  • Msanii huyo ambaye alinusurika kufa alieleza bayana kwamba aliona wazi Mungu akimpa nafasi nyingine ya kujirekebisha kimaisha na halichukulii hilo kwa wepesi.
  • Alitoa wito kwa msanii yeyote ambaye anahisi kazi yake ya muziki ni nzuri na angependa kufanya kazi ya kikoa na yeye kuwasiliana naye wakati huu ambapo yuko Kenya.

Jose Chameleone

MSANII Jose Chameleone kutoka Uganda amefichua kwamba ameacha matumizi ya pombe na sigara, si tu kwa sababu ya kukatazwa na madaktari lakini kwa sababu ya tathmini ya kikweli kuhusu afya yake.

Akizungumza na waandishi wa habari za burudani nchini Kenya alipotua katika angatua ya JKIA, Chameleone Alifichua kwamba ujio wake Kenya ni kwa ajili ya matibabu lakini pia kuwasalimia marafiki zake wa muda mrefu.

Msanii huyo ambaye amerudi Afrika kutoka Marekani alikokuwa akipokea msururu wa matibabu Alifichua kwamba amelazimika kuangalia upya mienendo ya afya yake bila hata kushauriwa na madaktari.

“Kabla niondoke kwenye USA nilikuwa nimepoteza takribani kilo 13. Na madaktari hawakunishauri nisifanye chochote, lakini nilitumia tathmini ya Kibinafsi.”

“Kuna baadhi ya vitu ambavyo sijakuwa nikifanya vizuri kwa afya yangu. Namaanisha nimekuwa nikimimina chupa mwilini mwangu, nimekuwa mvutaji sigara maisha yangu yote. Lakini kwa ajili ya kuboresha afya yangu nimesitisha hivyo vyote. Sasa hivi sivuti sigara wala sinywi pombe,” Chameleone alieleza.

Msanii huyo ambaye alinusurika kufa alieleza bayana kwamba aliona wazi Mungu akimpa nafasi nyingine ya kujirekebisha kimaisha na halichukulii hilo kwa wepesi.

“Hii ni raundi ya pili, Mungu amenipa awamu. Ya awali ilikuwa ya kwanza na sasa ninaanza ya pili. Na kumbuka nimesalia na miaka 3 kufikisha miaka 50, hivyo kuna baadhi ya vitu sharti nivipunguzie kasi,” Chameleone alisema.

Kuhusu kuendelea kimuziki, Chameleone alisema kwamba japo hajarudi kikamilifu katika maisha yake ya sanaa, bado ana uchu wa kuendelea ikiwa ni pamoja na kuwashika wasanii wengine mikono.

Msanii huyo ambaye taaluma yake ya muziki ilianzia Kenya takribani miaka 25 iliyopita Alifichua kwamba Kenya ina maana kubwa kwake kwani hata mpenzi wake wa kwanza alimpata akiwa Kenya.

Alitoa wito kwa msanii yeyote ambaye anahisi kazi yake ya muziki ni nzuri na angependa kufanya kazi ya kikoa na yeye kuwasiliana naye wakati huu ambapo yuko Kenya.

“Watu wengi hawajui lakini hata mpenzi wangu wa kwanza nilimpata nikiwa hapa Kenya. Vitu vingi sasna vilitokea kwangu kwa mara ya kwanza nikiwa Kenya, kutoka muziki hadi kila kitu.”

“Mimi ni hitmaker na kila mtu anajua hilo. Hivyo nini kingine ninaweza kufanya? Ni wakati wa kuwashika mikono watu wengine. Siko katika haraka ya kutoa hits, nimeshafanya hivyo kwa miaka mingi. Mimi naamini katika falsafa kwamba mwangaza wangu kusaidia wengine kupata nuru hakufifishi wangu,” alisema akikaribisha wasanii kumtafuta kufanya kazi.

 

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved