
ALIYEKUWA naibu rais Rigathi Gachagua amezungumzia dhana midomoni mwa wakenya wengi kwamba hawezi kuwania wadhifa wowote wa kisiasa nchini Kenya haswa baada ya kubanduliwa mamlakani Oktoba mwaka jana.
Akizungumza asubuhi ya Jumanne Februari 4 na stesheni za
jamii ya Abaluhya, Gachagua alisema kwamba hata kabla ya mchakato wa
kubanduliwa kwake, baadhi walimsihi kujiuzulu ili kunusuru mustakabali wake wa
kisiasa.
Alisema kwamba alikataa kujiuzulu kwa sababu hata hajipendi
kama ambavyo baadhi ya watu wanafikiria, akisema kwamba hata harakati zake sasa
hivi kupinga serikali si kwamba analenga kuwa chochote nchini.
Kiongozi huyo alifichua kwamba masaibu yake na rais Ruto
yalianza pale alipoamua kusimama na kumuambia ukweli wakati watu wengine karibu
naye walikuwa wanashindwa kumwambia.
“Yeye ndiye rais wa Kenya
na mimi nilikuwa msaidizi wake. Lakini hilo halikunitoa katika haki ya kuongea
kwa sababu pia mimi ni Mkenya na katiba inakubalia kila mtu kusema ukweli. Shida
ilikuwa kila mtu anaambia rais ‘ndio’ ile inaitwa Praise & Worship Choir,
mimi nilikataa kuingia katika hiyo kwaya nikiwa namwambia ukweli vile raia
wanasema,” Gachagua alisema.
“Mambo ya kwamba eti
nikifukuzwa sitasimama kiti hiyo haina maana kwangu. Mimi najua watu
wanafikiria kwamba mimi ni mtu najipenda sana, sio lazima niwe chochote katika
Jamhuri ya Kenya,” aliongeza.
Gachagua aliibua kauli yenye ukakasi kwamba rais Ruto hata
alifikia hatua ya kumuahidi shilingi bilioni 2 ili kujiuzulu badala ya kungoja
kung’atuliwa mamlakani, lakini akakataa.
“Na mimi hata
ningesikiliza vile rais alikuwa ameniambia nijiuzulu kwa sababu alikuwa
ameniambia ‘wewe jiuzulu nikupatie bilioni 2 uende nyumbani uende upumzike
ufanye mambo yako, ukuwe na walinzi, ukuwe na mshahara na unaweza simama siku
nyingine’…sasa nikajiuliza, yule anayekupangia mabaya anaweza kukupa suluhisho
jinsi utaishi?” alisema.
Gachagua alisema si rais tu alimrai kujiuzulu ili kuweka hai
mustakabali wake wa kisiasa, akisema kwamba hata baadhi ya wabunge wale
wanaomuunga mkono walimtaka kujiuzulu pia badala ya kungoja kubanduliwa.
“Waliniambia nijiuzulu
nikasema hiyo ni kujipenda, sio lazima nisimame, sio lazima niongoze, mimi
lazima nitetee wakenya na ukweli ujulikane,’ aliongeza.