logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Kebaso Aomba Karua Kumpa Kazi ya EACC Kama Atakuwa Rais Mbele Yake

“Kile kiti ambacho naomba unipe ni cha EACC. Mimi nataka kufanya kazi bila kulipwa, nipatie tu hiyo kazi na uzime simu uniache, nitawashughulikia [wezi],” Kebaso alisema.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Habari27 February 2025 - 14:51

Muhtasari


  • Akionesha uchu wake wa kutumbua majipu katika idara mbalimbali za serikali, Kebaso alisema kwamba atanyoosha kila idara ya suala la ufisadi litakuwa la kusikika tu.
  • Karua amezindua upya chama chake baada ya kukibadilisha jina kutoka NARC-K mwezi uliopita hadi PLP.

Martha Karua na Morara Kebaso

MWANAHARAKATI na mwanasiasa Morara Kebaso amemuomba kiongozi wa chama cha People’s Liberation Party, Martha Karua kumteua kama mkuu wa Tume ya Maadili na Kupambana na Rushwa EACC iwapo atakuwa rais mbele yake.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa chama hicho cha PLP jijini Nairobi, Kebaso ambaye ni Mwanzilishi wa chama cha INJECT alisema kwamba Kenya imejawa na ufisadi na ubadhirifu wa fedha za umma haswa chini ya utawala wa rais William Ruto.

Kebaso alisema kuwa pia yeye analenga kuwa rais wa Kenya lakini akamuomba Karua iwapo atatangulia kuwa rais mbele yake, basi asisite kumteua kama mkuu wa EACC.

Akionesha uchu wake wa kutumbua majipu katika idara mbalimbali za serikali, Kebaso alisema kwamba atanyoosha kila idara ya suala la ufisadi litakuwa la kusikika tu.

“Nimekuwa na bahati ya kutembea katika Maeneo mbalimbali humu nchini, jumla ya kaunti 32, na mheshimiwa [Martha Karua] mimi nataka kukuambia kwamba yale mambo yanaendelea hapa ni wizi mtupu bila kazi. Ni wizi kulia, kushoto na kati.”

“Hakuna kitu cha maana kinachoendelea katika taifa letu. Katika bajeti ya trilioni 3.9, asilimia 70 inaenda katika wizi na ubadhirifu wa fedha za umma. Na kama utaenda popote humu nchini, ni miradi iliyokwama baada yam ingine. Ufisadi umeua ugatuzi wetu, umemaliza fursa za vijana.”

“Mimi nina azma ya kuwa rais wa Kenya, lakini hilo ni kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu. Ni Mungu anapatiana uongozi, sio mimi wa kujipa mwenyewe. Kama utakuwa rais mbele yangu, kile kiti ambacho naomba unipe ni cha EACC. Mimi nataka kufanya kazi bila kulipwa, nipatie tu hiyo kazi na uzime simu uniache, nitawashughulikia [wezi],” Kebaso alisema.

Karua amezindua upya chama chake baada ya kukibadilisha jina kutoka NARC-K mwezi uliopita hadi PLP.

Katika hafla hiyo ya uzinduzi upya, kando na Kebaso, wanasiasa wakuu wengine ambao walikuwepo ni pamoja na aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua, kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka miongoni mwa wengine.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved