
Wakili na mwanasiasa wa Kenya Martha Karua kwa sasa yuko nchini Uganda ambako anahudhuria kikao cha mahakama cha kiongozi wa upinzani Kizza Besigye.
Wakili huyo mwenye uzoefu wa miaka mingi hata hivyo amefichua kwamba haruhusiwi kumtetea Besigye na washtakiwa wenzake mahakamani jinsi alivyokusudia. Hii, anasema, ni kwa sababu ya idhini iliyodhibitiwa ya leseni yake maalum.
"Niko mahakamani lakini sina sauti kutokana na hali ya kizuizi cha leseni yangu maalum," Karua alisema siku ya Jumatano asubuhi kupitia X.
Licha ya kuzuiwa kumtetea mteja wake, kiongozi huyo wa chama cha PLP hata hivyo amewapongeza wenzake kwa kazi nzuri wanayofanya.
Pia amefichua kuwa yuko mbioni kuomba tena leseni nyingine maalum.
Mapema mwezi uliopita, Baraza la Sheria la Uganda hatimaye lilimpatia Martha Karua cheti cha muda cha kazi ambacho kingemruhusu kumwakilisha mwanasiasa wa Upinzani aliyezuiliwa Kizza Besigye.
Karua alipokea cheti hicho baada ya kutuma ombi tena kupitia Chama cha Wanasheria cha Uganda.
“Baraza la Sheria limempatia Cheti cha kazi cha muda Mhe. Martha Karua, kufuatia maombi yake tena kupitia Chama cha Wanasheria wa Uganda, kama ilivyoagizwa na Rais wetu wa #RadicalNewBar, Isaac Ssemakadde,” Chama cha Wanasheria wa Uganda kilisema kwenye taarifa.
Haya yalitokea takriban wiki nne baada ya
kunyimwa leseni ya mazoezi na Baraza la Sheria la Uganda.
Karua ndiye wakili mkuu katika kesi ya Kizza Besigye kufuatia madai ya kutekwa nyara nchini Kenya na baadaye alifikishwa katika mahakama ya kijeshi nchini Uganda, pamoja na rafiki yake Obeid Lutale.
Aidha alisema baraza lilimweleza kuwa nyaraka za uraia na sifa za kitaaluma haziambatanishwa na maombi yake, pamoja na yale ya Erias Lukwago, wakili mwingine anayemwakilisha Besigye.