
Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen alikutana na maafisa wa polisi Jumatano saa kumi na moja alfajiri jijini Nairobi.
Mkutano huo ulikuwa na lengo la kuhakikisha usalama wa wananchi huku nchi ikijiandaa kuadhimisha kumbukumbu ya mwaka mmoja tangu maandamano ya Julai 25.
Hii inajiri siku moja baada ya Murkomen kujibu baadhi ya watu waliotishia kuvamia Ikulu.
Akizungumza katika Ikulu ya Nairobi, Jumanne, Juni 24, 2025, Murkomen alisema kuwa ni Kenya pekee ambapo watu huruhusiwa kutembea huru baada ya kutangaza nia ya kuvamia Ikulu au hata Bunge la Kitaifa.
Murkomen alidai kuwa katika mataifa mengine, vitisho vya aina hiyo havivumiliwi.
“Ni Kenya pekee ambapo mtu huandika kwenye mitandao ya kijamii kwamba atavamia Ikulu, mahakama au bunge. Na hata wakipelekwa mahakamani, wataachiliwa na kuambiwa waende nyumbani bure, na hakuna chochote kinachowapata,” alisema wakati wa kiamsha kinywa na mabingwa wa Ligi Kuu ya FKF kilichofanyika Ikulu tarehe 24 Juni 2025.
Aidha, Murkomen alisema kuwa watu wanaotoa vitisho vya aina hiyo wangekamatwa na kufunguliwa mashtaka katika nchi kama Uingereza na Marekani.
“Kwa mfano, nchini Uingereza, mtu yeyote akiandika au kuchapisha kwenye mitandao ya kijamii kwamba atazuru Kasri la Buckingham au Bunge, hakuna atakayengoja atokee mitaani; atachukuliwa kutoka nyumbani kwake na kufunguliwa mashtaka. Mmarekani akiandika kuwa atavamia Ikulu ya Marekani, Secret Service itatumwa nyumbani kwake,” aliongeza.
Vilevile, Murkomen amewataka polisi wawe wakali wanapokabiliana na wahuni wakati wa maandamano yaliyopangwa.
Kwa mujibu wa Murkomen, serikali haitakaa kimya na kushuhudia waandamanaji waliojihami wakisababisha vurugu katika eneo la kibiashara la Nairobi (CBD).
“Tumepokea taarifa kutoka kwa baadhi ya wanasiasa ambao, si miezi mingi iliyopita, walikuwa wakitetea sheria na utulivu, walikuwa dhidi ya vurugu, lakini sasa wanapanga kununua mapanga na marungu, wakijaribu kuwagawia vijana ili wasababisha machafuko mjini. Na wanataka tuketi hapa na kukunja mikono tukisema hiyo ni Ibara ya 137 ya katiba,” alisema.
“Polisi wa kitaifa lazima wawe wakali wanapokabiliana na wahalifu wa aina hiyo kwa sababu tunataka nchi hii iwe ya sheria na utulivu, si ya vurugu, ili kila mmoja aweze kustawi,” aliongeza.
Viongozi wa upinzani na makundi ya vijana wameapa kurejea mitaani kwa heshima ya waliopoteza maisha wakati wa maandamano ya mwaka 2024.