logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Kilichosababisha kifo cha mwanaharakati wa Molo Richard Otieno chafichuliwa

Oduor alisema kuwa silaha iliyotumiwa kumsababishia Otieno majeraha kichwani inaweza kuwa shoka au panga.

image
na Samuel Mainajournalist

Yanayojiri25 January 2025 - 10:18

Muhtasari


  • Oduor amethibitisha kwamba Richard Otieno alifariki kutokana na majeraha ya kichwa yaliyosababishwa na kifaa chenye ncha kali.
  • Familia ya Otieno, ambao walikuwa miongoni mwa waliokuwepo wakati wa uchunguzi wa maiti, walidai haki kwa mpendwa wao.



Mwanapatholojia mkuu wa serikali Dkt Johansen Oduor amethibitisha kwamba mwanaharakati wa Molo aliyeuawa ,Richard Otieno, alifariki kutokana na majeraha ya kichwa yaliyosababishwa na kifaa chenye ncha kali.

Otieno aliuawa nje ya nyumba yake katika mji wa Elburgon, kaunti ya Nakuru, usiku wa Jumamosi, Januari 18, na watu wasiojulikana.

Akizungumza na waandishi wa habari Ijumaa, Oduor alisema kuwa silaha iliyotumiwa kumsababishia Otieno majeraha kichwani inaweza kuwa shoka au panga.

"Kulikuwa na majeraha kadhaa mabaya, ikiwa ni pamoja na majeraha mengi ya kukatwa sehemu ya nyuma ya kichwa, ambayo yalisababisha kuvunjika kwa fuvu na kuvuja damu nyingi kwenye ubongo," Oduor alisema.

Mwanapatholojia huyo alisema hayo baada ya kufanya uchunguzi wa maiti siku ya Ijumaa katika chumba cha kuhifadhi maiti cha Hospitali ya Kericho County Level Five.

"Pia kulikuwa na majeraha ya kukatwa sehemu ya mbele ya fuvu la kichwa, ingawa hayakusababisha kuvunjika," aliongeza.

Otieno ambaye alikuwa mkosoaji mkali wa serikali, alijulikana kama 'Rais wa Molo'.

Aliuawa kwa kukatwakatwa siku mbili baada ya kulalamika kuwa alikuwa akipokea vitisho na kuandamwa na watu watatu wasiojulikana.

Mwanaharakati huyo aliyezungumza waziwazi alipatikana ameuliwa karibu na nyumba yake, mita chache kutoka kituo cha polisi cha Elburgon.

Oduor alisema walikusanya sampuli kutoka kwa mwili wake kwa uchunguzi zaidi.

 "Watu wawili wanapohusika katika ugomvi mkali, mara nyingi hubadilishana nyenzo za DNA. Sampuli zitakazokusanywa zitasaidia kuwatambua wahusika. Pia tulikusanya sampuli za kucha kwa ajili ya uchunguzi wa DNA ili kubaini iwapo marehemu alikuwa na kitu chochote kabla ya kukutana na washambuliaji wake," alieleza.

Maafisa wa upelelezi kutoka Idara ya uchunguzi wa Mauaji ya DCI wanashughulikia kesi hiyo ili kubaini waliohusika na mauaji hayo ya kutatanisha.

Familia ya Otieno, ambao walikuwa miongoni mwa waliokuwepo wakati wa uchunguzi wa maiti, walidai haki kwa mpendwa wao.

Wengine waliokuwepo wakati wa zoezi hilo ni mwanasheria wa familia na maafisa kutoka Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu ya Kenya (KNCHR).


Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved