logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Ngome yatikisika? Raila apokewa vibaya Kisii baada ya makubaliano na Ruto

Raila alikumbana na mapokezi mabaya katika Uwanja wa Gusii katika kaunti ya Kisii alipohudhuria hafla ya kandanda.

image
na Samuel Mainajournalist

Yanayojiri10 March 2025 - 07:31

Muhtasari


  • Raila aliposimama kuhutubia mashabiki, sehemu ya umati ilianza kumzomea kwa kauli ya "Raila must go!" 
  •  Wengine walionyesha kutoridhishwa kwa kuondoka uwanjani.

Mashabiki waondoka katika uwanja wa Gusii baada ya Raila Odinga kusimama kuzungumza mnamo Machi 9, 2025.

Kiongozi wa ODM, Raila Odinga, mnamo siku ya Jumapili alikumbana na mapokezi mabaya katika Uwanja wa Gusii katika kaunti ya Kisii alipohudhuria hafla ya kandanda.

Raila alikuwa amezuru Kisii kwa ajili ya kushudia kutiwa saini mkataba wa udhamini wa Sportspesa na Shabana FC, ingawa hakuwa na hakika kama angepokewa vizuri.

Mara tu Waziri Mkuu huyo wa zamani aliposimama kuhutubia mashabiki, sehemu ya umati ilianza kumzomea kwa kauli ya "Raila must go!"

Wengine walionyesha kutoridhishwa kwa kuondoka uwanjani.

Hata hivyo, Raila aliendelea na hotuba yake bila kuyumbishwa na malalamiko hayo.

Hatua hii inaonekana kuchochewa na hatua ya ODM kusaini makubaliano (MoU) na chama cha UDA cha Rais William Ruto—uamuzi ambao umewaghadhabisha baadhi ya viongozi na wafuasi wa ODM.

Eneo la Kisii kwa muda mrefu limekuwa likichukuliwa kama ngome ya Raila, jambo linalofanya tukio hili kuwa la kipekee.

Hatua ya kusaini makubaliano hayo ilitanguliwa na mashauriano ya Raila na wanachama wa chama chake katika ngome zake za kisiasa, akitafuta maoni kuhusu mwelekeo wake wa kisiasa.

Wiki iliyopita, kinara huyo wa ODM na rais William Ruto waliingia rasmi katika makubaliano ya kisiasa yatakayoshuhudia vyama vyao vikishirikiana.

Mkataba wa Ushirikiano kati ya Kenya Kwanza na ODM ulisainiwa Ijumaa katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Kenyatta (KICC) jijini Nairobi, kwenye hafla iliyohudhuriwa na Wabunge wanaomuunga mkono kila kiongozi.

Naibu Rais Kithure Kindiki pia alihudhuria hafla hiyo.

Kupitia mkataba huu, vyama vya UDA na ODM vitashirikiana katika masuala ya kitaifa kwa kutumia miundombinu yao ya kisiasa.

Pia, vyama hivyo vitawatumia wataalamu wao mahiri kwa mashauriano kuhusu utawala na sera za kitaifa.

Kabla ya hafla ya utiaji saini, maelfu ya wafuasi wa ODM walikusanyika katika KICC kushuhudia tukio hilo la kihistoria.

Hafla hiyo ilifuatia mfululizo wa mashauriano ambayo kiongozi wa ODM Raila Odinga alifanya katika maeneo mbalimbali nchini ambako ana uungwaji mkono mkubwa wa kisiasa.


Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved