
Kiungo wa zamani wa Harambee Stars, Victor Wanyama,
amesajiliwa na klabu ya Daraja la Pili Scotland, Dunfermline Athletic FC, kwa
mkataba wa muda mfupi hadi mwishoni mwa msimu huu, akisubiri kibali cha
kimataifa.
Wanyama, mwenye umri wa miaka thelathini na mitatu, anarejea katika soka la Scotland na kuungana tena na kocha Neil Lennon, aliyewahi kumnoa akiwa Celtic kati ya mwaka 2011 na 2013. Katika kipindi hicho, Wanyama alishinda mataji mawili ya ligi kuu ya Scotland na Kombe la FA la nchi hiyo, huku akijizolea sifa kwa kufunga bao muhimu katika ushindi wa kihistoria wa Celtic dhidi ya Barcelona kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya mwaka 2012.
Baada ya kuondoka Celtic kwa uhamisho wa pauni milioni 12.5 kwenda Southampton, Wanyama alicheza misimu mitatu akiwasaidia Saints kumaliza katika nafasi ya nane, saba na sita kwenye Ligi Kuu ya Uingereza, hivyo kufuzu kwa mashindano ya bara Ulaya. Kisha alihamia Tottenham Hotspur mwaka 2016, ambako alidumu kwa misimu minne kabla ya kujiunga na CF Montreal ya Canada mwaka 2020.
Baada ya mkataba wake na Montreal kumalizika Januari mwaka huu, kiungo huyo mwenye uzoefu mkubwa sasa atasaidia Dunfermline Athletic kupambana kusalia kwenye ligi. Kikosi hicho kinashikilia nafasi ya tisa kwenye msimamo wa Daraja la Pili Scotland, kikiwa na tofauti ya pointi sita kutoka mkiani na pointi mbili nyuma ya Hamilton waliopo nafasi ya nane.
Kocha Neil Lennon, aliyeteuliwa wiki iliyopita, ana kibarua
kigumu cha kuokoa klabu hiyo na mechi yake ya kwanza itakuwa dhidi ya Ayr
United inayonolewa na Scott Brown, mchezaji mwenzake wa zamani wa Celtic. Ikiwa
atakuwa tayari kimwili, Wanyama huenda akapewa nafasi ya kucheza katika mechi
hiyo muhimu.
Kwa kurejea Scotland, Wanyama anapata fursa nyingine ya kuonyesha uwezo wake katika soka la Ulaya.
Licha ya kuwa katika daraja la pili, ushawishi wake na uzoefu
wake wa kimataifa unaweza kuwa msaada mkubwa kwa Dunfermline, huku akitarajiwa
kuleta uthabiti na uongozi uwanjani wakati timu hiyo inapambana kuepuka kushushwa
daraja.