logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mwangaza ajipata gizani, mahakama yaidhinisha kubanduliwa kwake

Jaji Bahati Mwamuye siku ya Ijumaa alitupilia mbali ombi la Mwangaza akieleza kuwa mchakato wa kumfurusha ulifuata taratibu za kisheria.

image
na Davis Ojiambo

Mahakama14 March 2025 - 16:17

Muhtasari


  • Gavana Mwangaza alikuwa amepinga kuondolewa kwake madarakani akiibua sababu mbalimbali
  • Jumla ya maseneta 26 walipiga kura kuunga mkono mashtaka matatu yaliyofikishwa dhidi ya Bi Mwangaza.
  • Kawira hata hivyo anatarajiwa kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa mahakama kuu.

Gavana wa Meru Kawira Mwangaza

Mahakama kuu imeidhinisha kuondolewa afisini kwa kwa Gavana wa Meru Kawira Mwangaza ikisema mchakato uliopelekea kuondolewa kwake ulifuata sheria.

Jaji Bahati Mwamuye siku ya Ijumaa alitupilia mbali ombi la Mwangaza akieleza kuwa mchakato wa kumfurusha ulifuata taratibu za kisheria.

"Ombi lililorekebishwa la Desemba 23, 2024, halijafikia kiwango cha kisheria kinachohitajika kwa mahakama hii kubatilisha uamuzi wa Seneti," jaji alitoa uamuzi huku akitupilia mbali ombi la Mwangaza.

"Ilani ya gazeti la serikali ya Agosti 20, 2024, iliyotolewa na Seneti ikiwasilisha uamuzi wa kumwondoa mlalamishi afisini kama gavana wa Meru, mashtaka yamethibitishwa," Jaji Mwamuye aliamua.

Gavana Mwangaza alikuwa amepinga kuondolewa kwake madarakani akiibua sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na madai ya ukiukwaji wa taratibu, kusikilizwa kwa haki na madai ya kutoshirikishwa ipasavyo kwa umma.

Bi Mwangaza alikuwa mmoja wa magavana saba wa kike waliochaguliwa baada ya uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022 huku akijizolea kura 209,148 na kumwangusha aliyekuwa gavana Kiraitu Murungi na aliyekuwa Waziri wa Kilimo Mithika Linturi.

Jumla ya maseneta 26 walipiga kura kuunga mkono mashtaka matatu yaliyofikishwa dhidi ya Bi Mwangaza.

Lakini alikimbilia kortini siku iyo hiyo na Jaji Mwamuye akasimamisha utekelezaji wa azimio la Seneti, kumwondoa afisini.

Bunge la Seneti lilipinga agizo la kusitisha kuondolewa kwake likisema kwamba agizo hilo lilikuwa linaingilia mamlaka ya maseneta.

Seneti pia lilisema kwamba halikupewa fursa ya kusikilizwa kabla ya agizo hilo kutolewa. Maseneta walisema agizo hilo lilikuwa linakiuka kanuni za haki asilia, ambazo zinahitaji kwamba pande zote zina haki ya kusikilizwa kabla ya uamuzi wowote kutolewa.

Kawira hata hivyo anatarajiwa kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa mahakama kuu.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved