
Mbunge wa Mumias Mashariki Peter Salasya amejitokeza tena na kuweka wazi kiwango anachopata cha mshahara.
Akichapisha na kuweka wazi maelezo ya mshahara wake katika mtandao wake wa instagram Salasya alisikitia pakubwa jinsi mshahara wake ulivyokatwa kwa kugharamia ushuru mbalimbali, kulingana na maelezo ya bwana Salasya alidokeza kuwa yeye hupokea kiwango cha mshahara wa zaidi ya shilingi milioni moja na laki moja 1.1m.
Kulingana na Salasya kwa sasa yeye hupeleka nyumbani mshahara wa shilingi elfu kumi na nane pekee baada ya makato kufanyika, alielezea akisema kuwa kati ya makato ambayo hufanywa ni kugharamia pesa za hazina ya pesa za uzeeni NSSF,ushuru wa kugharamia bima ya matibabu,ushuru wa kugharamia nyumba za ujenzi wa bei nafuu miongoni mwa makato mengine.
Salasya alionekana kumunyoshea kidole cha lawama rais Ruto kwa kuzindua sera dhalimu na za kumfyonza raia na wafanyakazi pesa kila uchao kwa kigezo cha kutoa ushuru kujenga Kenya ya baadaye ''watu wamejitolea na kujikaza kukatwa mishahara yao ila Rais ananyemelea mishahara yao na kuongeza kodi za ushuru mara kwa mara,'' kama mimi huo ndio mshahara wangu sembuse mwalimu ,daktari au askari'' Salasya alikariri.
Mbunge Salasya alifafanua kuwa yeye hupokea jumla ya mshahara wa shilingi 435,301, marupurupu ya afisi yake ya shilingi 140,201 marupurupu ya nyumba 150,000, marupurupu ya kufanya kazi ya 150,000 na marupurupu ya muda wa mawasiliano ya shilingi 15,000.
Mbunge huyo wa Mumias mashariki alifafanua hayo yote akiwa na nia ya kuwafahamisha wakenya jinsi hata wao wanavyonyogwa na sera dhalimu za serikali tawala akisema kuwa hii hali imewafanya wakenya wengi kuishi katika maisha ya kujuta na kuhangaika kwa sababu ya kukosa pesa za kuwasaidia kujikimu kimaisha.
Itakumbukwa wazi kuwa juma lililopita wakati wa ziara ya raisi eneo la magharibi bwana salasya alipopewa fursa ya kuhutubia umma alimweleza rais peupe kuwa mpango wa bima ya matibabu haukuwa ukifanya kazi licha ya watu wengi hasahasa wandani wa rais wa karibu kukosa kumueleza'' bwana rais uko na watu wengi ambao wako karibu na wewe ila huwa hawakuelezi kuwa SHA haifanyi kazi hawakuambiii ukweli bwana rais'' salasya alidokeza.
Peter Salaya kwa mara nyingi ameonekana akikosoa serikali ya Kenya kwanza kwa kutotimiza ahadi zake na kuendelea kumfyonza kimfuko mwananchi wa kawaida Salasya aliyechaguliwa kwa tiketi ya chama cha DAP-Kenya chake Eugine Wamalwa anaonekana kuwa mtetezi mkubwa wa wananchi licha ya kuwa mbunge mchanga tena aliyechaguliwa kwa mara ya kwanza bungeni.