
Mwanawe Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, amekanusha madai ya muda mrefu kwamba mama yake, Janet Kataha Museveni, aliwahi kuwa na uhusiano wa kimapenzi na kiongozi wa upinzani, Kizza Besigye.
Kwa miaka mingi, kumekuwa na uvumi kwamba Janet Museveni aliwahi kuwa mpenzi wa Besigye kabla ya kufunga ndoa na Rais Museveni. Wanasiasa hao wawili walikuwa marafiki wakubwa na walifanya kazi pamoja kabla ya uhusiano wao kuvunjika zaidi ya miongo miwili iliyopita.
Siku ya Jumanne, mtumiaji mmoja wa mtandao wa X aliibua upya madai hayo alipokuwa akijibu moja ya tweet za Muhoozi. Alidai kwamba Janet aliwahi kuwa mpenzi wa Besigye na hata kudai kuwa Muhoozi huenda ni mtoto wa kiongozi huyo wa upinzani badala ya Museveni.
"Lakini mama yako ni mpenzi wa zamani wa Besigye. Huenda wewe ni mtoto wa Besigye, si wa Museveni," aliandika mtumiaji huyo wa X.
Muhoozi, ambaye ni Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi wa Uganda, alikanusha vikali madai hayo na hata kusema kwamba angejitoa uhai iwapo yangekuwa ya kweli kwa kiwango chochote.
"Hilo haliwezekani! Lakini kama kungekuwa na hata asilimia 0.0001 ya ukweli, ningejitoa uhai mara moja," Muhoozi alijibu.
Muhoozi aliendelea kumsifu mama yake, ambaye pia ni Waziri wa Michezo na Elimu wa Uganda, akimtaja kama mwanamke wa pili mrembo zaidi duniani, baada ya mke wake, Charlotte Kainerugaba.
"Huyo ndiye Janet Kataha Museveni, mama yangu. Mwanamke wa pili mrembo zaidi duniani! Baada ya Charlotte Kainerugaba," alisema.
Katika miaka ya hivi karibuni, Muhoozi ameonyesha wazi chuki yake kwa Besigye. Mahusiano yao yamekuwa na mvutano mkubwa, huku mzozo wao wa hivi karibuni ukitokea Februari 2025.
Wakati huo, Muhoozi alimshambulia mke wa Besigye, Winnie Byanyima, kwa sababu ya uhusiano wake wa zamani na Museveni. Byanyima alikuwa amekiri kwenye mahojiano ya redio kwamba walikuwa na uhusiano wa kawaida, lakini Muhoozi alipinga kauli hiyo, akimshutumu kwa kujaribu kuvuruga familia yake na kudai kwamba Museveni alimaliza uhusiano huo mnamo 1986.
Kwa kujibu, Byanyima alimwonya Muhoozi dhidi ya kupotosha historia, akidokeza kuwa ana ushahidi wa kuweka wazi ukweli kuhusu uhusiano wake wa zamani na Museveni.
Mvutano huu ulitokea wakati Besigye akikabiliwa na matatizo ya kisheria.
Kiongozi huyo wa upinzani alikamatwa Novemba 2024, ambapo inadaiwa alitekwa nyara kutoka Kenya na kupelekwa Uganda, ambako anakabiliwa na kesi ya kijeshi kwa mashtaka ya uhaini na umiliki haramu wa silaha.