logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Nimefarijika Kuona Mume Wangu Akitembea na Kuzungumza Tena – Mkewe Besigye

Hakimu alimuru kuzuiliwa kwake hadi Machi 7 wakati kesi yake inatarajiwa kusikilizwa, hatua ambayo ilimpelekea Besigye kumaliza mgomo wake dhidi ya chakula.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Kimataifa04 March 2025 - 14:01

Muhtasari


  • Katika chapisho hilo, Byanyima alieleza kwamba Kizza Besigye sasa anaweza kutembea tena na kuzungumza na watu wanaomtembelea gerezani.
  • Besigye alikuwa amezuiliwa kizuizini tangu mwaka jana baada ya kutekwa nyara jijini Nairobi Kenya na kusafirishwa kinyemela hadi nchini Uganda.

Winnie Byanyima na mumewe Kizza Besigye

WINNIE Byanyima, mkewe mwanasiasa wa muda mrefu katika siasa za mrengo wa upinzani nchini Uganda amedokeza kwamba hali ya afya ya mumewe ambaye yuko kizuizini inaendelea kuimarika.


Byanyima, ambaye aliwahi kuwa mpenzi wa rais wa sasa Yoweri Museveni alitoa sasisho hilo kupitia ukurasa wake wa X baada ya kumtembelea mumewe katika gereza la Luzira anakozuiliwa pamoja na wakili wake Haji Obeid Lutale.


Katika chapisho hilo, Byanyima alieleza kwamba Kizza Besigye sasa anaweza kutembea tena na kuzungumza na watu wanaomtembelea gerezani.


“Nilitembelea @kizzabesigye1 na Haji Obeid Lutale katika Gereza la Luzira leo. Wote wawili walikuwa na roho nzuri. Nilifarijika kuona @kizzabesigye1 anaweza kutembea na kuzungumza na wageni wake,” mkewe aliandika.


Pia alitumia fursa hiyo kutoa wito kwa mahakama kusikiliza kesi hiyo na kumpa dhamana mumewe, akisema kwamba Besigye amekuwa mtiifu wa kuhudhuria vikao vya mahakama kwa kesi zake kwa miaka 20 sasa.


“Baada ya miaka 20 ya kufika mahakamani kwa uaminifu kwa mashtaka mengi ya jinai, HAKUNA sababu ya kukataa kumpa @kizzabesigye1 dhamana. Jaji lazima asikilize maombi yake na kukomesha dhuluma hii. Inatosha!” alifoka.


Besigye alikuwa amezuiliwa kizuizini tangu mwaka jana baada ya kutekwa nyara jijini Nairobi Kenya na kusafirishwa kinyemela hadi nchini Uganda.


Baada ya mamlaka kukata kuhamisha kesi yake hadi katika mahakama ya kiraia na kuamua kumfungulia mashtaka katika mahakama ya kijeshi, mwanasiasa huyo alianza mgomo wa kususia chakula.


Kutokana na hali hiyo, alidhoofika kwa kiasi kikubwa kiasi kwamba alishindwa kutembea na kuzungumza hadi kupelekwa mahakamani akiwa kwenye kiti cha magurudumu.


Mnamo Februari 21, Besigye alihamishiwa katika mahakama ya kiraia na kufunguliwa mashtaka na jinai ambayo adhabu yake ni kifo.


Hakimu alimuru kuzuiliwa kwake hadi Machi 7 wakati kesi yake inatarajiwa kusikilizwa, hatua ambayo ilimpelekea Besigye kumaliza mgomo wake dhidi ya chakula.


Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved