Willis Raburu aondoka TV47 miezi baada ya kupandishwa cheo

Raburu anaondoka Cape Media baada ya takriban miezi 8.

Muhtasari

•Kuondoka kwake kunakuja miezi kadhaa baada ya kuteuliwa kama Mkurugenzi wa Huduma za Dijitali na Ubunifu.

•Raburu alijiunga na TV47 mwaka wa 2023, hatua iliyowasisimua mashabiki wake. 

Willis Raburu katika studio za Radio Jambo
Image: RADIO JAMBO

Mwanahabari mashuhuri Willis Raburu ameondoka rasmi katika Cape Media inayomiliki TV na Radio 47.

Raburu anaondoka Cape Media baada ya takriban miezi 8. Kuondoka kwake kunakuja miezi kadhaa baada ya kuteuliwa kama Mkurugenzi wa Huduma za Dijitali na Ubunifu.

"Ninapoiaga familia ya TV47, ninajawa na hisia ya fahari na shukrani kwa ukuaji wa ajabu ambao tumefikia pamoja katika miezi michache iliyopita," sehemu ya ujumbe wake wa kuaga inasoma.

Juzi tu, Willis alitangaza kuwa kipindi chake cha 'Wabebe Experience' kilikuwa kinachukua mapumziko kutoka hewani. Alikuwa mtangazaji mkuu wa kipindi hicho pamoja na Mc Gogo na Claudia Naisabwa.

"Tungependa kutangaza kwamba Wabebe Experience itachukua MUDA WA KUPUNGUA KWA MSIMU. Tunawashukuru kwa dhati watazamaji wetu kwa usaidizi wao endelevu na shauku

Uwe na uhakika, tunafanya kazi kwa bidii nyuma ya pazia ili kurudi KWA UKUBWA NA UBORA zaidi kuliko hapo awali. Endelea kufuatilia kwa sasisho za kurudi kwetu! Tunakupenda na tunakuthamini sana."

Raburu alijiunga na TV47 mwaka wa 2023, hatua iliyowasisimua mashabiki wake. Mnamo Agosti 22, aliwafahamisha mashabiki kwamba alikuwa karibu kutangaza jambo jipya.

Baadaye iliibuka kuwa atakuwa akiandaa kipindi kipya kilichopewa jina la Wabebe XP (uzoefu) kwenye TV47 kila Ijumaa saa nne usiku.

Alikuwa mtangazaji pamoja na Mc Gogo. Claudia Naisabwa kisha alijiunga nao Februari 2024 kama mwenyeji wa tatu.