Thee Pluto na mpenziwe watarajia mtoto wa kwanza pamoja, wafichua sababu za kuficha ujauzito

Wawili hao walilazimika kutangaza ujauzito huo kufuatia shinikizo kutoka kwa mashabiki.

Muhtasari

•Wawili hao walitangaza habari kuhusu ujauzito wao katika video iliyopakiwa kwenye YouTube channel ya Felicity.

•Thee Pluto alisema kuwa awali walisita kufichua ujauzito kwa kuwa hawakutaka watu kuingilia mahusiano yao.

Image: INSTAGRAM// FELICITY SHIRU

Wapenzi maarufu Robert Ndegwa (Thee Pluto) na Felicity Wanjiru wanatarajia mtoto wao wa kwanza pamoja.

Wawili hao walitangaza habari kuhusu ujauzito wao katika video iliyopakiwa kwenye YouTube channel ya Felicity.

Hatua hii ilifuatia shinikizo kubwa kutoka kwa mashabiki wao waliowataka kuzungumzia suala hilo baada ya wengi kumshuku kipusa huyo mwenye umri wa miaka 22  kuwa mjamzito.

"Tuko na sababu kadhaa kwa nini hatukuta kutangaza mapema. Sababu zangu ni kuwa hata kama tulijitambulisha hadharani kama wapenzi, pia nilitaka faragha yangu kidogo. Awali hata hatukufaa kutangaza. Lakini alinishawishi," Thee Pluto alisema baada ya mpenzi wake kufichua tumbo lake lililojitokeza.

YouTuber huyo alieleza kuwa awali walisita kufichua ujauzito kwa kuwa hawakutaka watu kuingilia mahusiano yao na hatimaye kuwatenganisha.

Kwa upande wake Felicity alisema alilazimika kutangaza kwa kuwa yeye ni mtu anayetanganana na wengine sana na hatimaye angekutana na watu ambao wangemuuliza maswali mengi baada ya kuliona tumbo lake.

"Awali nilikuwa sitaki kutangaza. Nilipendelea kuiweka siri," Alisema.

Watakapobarikiwa na mtoto wao, wawili hao watajiunga na orodha ya wapenzi wadogo mashuhuri ambao tayari ni wazazi. Wengine ni Tyler Mbaya (Baha) na mpenziwe Georgina Njenga, Masilver wa Sailors Gang na mpenziwe Winny Wayua pamoja na wengine.

Mtoto atakayezaliwa hatakuwa wa kwanza wa Thee Pluto. Mwanafunzi huyo katika chuo kikuu cha JKUAT ana mtoto wa kike mwenye umri wa miaka miwili pamoja na mpenzi wake wa zamani.

Thee Pluto hata hivyo hana uhususiano mzuri na mzazi mwenzake, suala ambalo amewahi kuzungumzia mara kadhaa.

Mwishoni mwa mwaka jana, YouTuber huyo alifichua kuwa familia ya baby mama wake ilimnyima ruhusa kuonana na binti yake.

Pluto alikuwa ameandaa karamu ya gharama kubwa ili kusherehekea ushindi wake katika umri mdogo kama huo.

Kulingana naye, alitaka kutumia karamu hiyo kumtambulisha binti yake mrembo kwa familia na marafiki zake.

Lakini cha kusikitisha ni kwamba familia ya mtoto wa mamake ilifutilia mipango hiyo dakika ya mwisho na hawakufanikiwa.

"Saa tano subuhi, upande wa msichana ulirudi nyuma, ilibidi niende huko mwenyewe," Pluto alisema katika mahojiano.