“Angetafuta yake kwanza!” Samidoh ajibu vikali madai alipewa HSC kwa sababu ya Karen Nyamu

Mwimbaji huyo alitaja mafanikio yake makubwa kutokana na Mungu na mashabiki wake.

Muhtasari

•Samidoh alimshukuru rais William Ruto kwa kumtambua na akaahidi kuendelea kuweka juhudi zaidi katika tasnia hiyo.

•Mashabiki walipendekeza Karen Nyamu alikuwa na jukumu la kutekeleza katika uteuzi wa wale waliotambuliwa.

Karen Nyamu na mpenzi wake Samidoh
Image: FACEBOOK// KAREN NYAMU

Siku ya Jumatano, mwimbaji tajika wa Mugithi Samuel Muchoki almaarufu Samidoh alishuhudia makumi ya wanamitandao wakimtaja mzazi mwenzake na mpenzi wake, Karen Nyamu kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii baada ya kushiriki habari njema kuhusu yeye kutambuliwa na rais katika tuzo za mkuu wa nchi za kila mwaka mnamo siku ya Jamhuri.

Katika taarifa, mwanamuziki huyo ambaye pia ni afisa wa polisi alisherehekea kutambuliwa kwake na rais William Ruto katika Sikukuu ya Jamhuri ya mwaka huu na akajivunia safari yake ya unyenyekevu ya mafanikio.

Wakati huohuo, alitaja mafanikio yake makubwa kutokana na Mungu na mashabiki wake.

‘Leo, nachukua muda kutoa shukrani zangu kwa Mwenyezi Mungu kwa safari ya ajabu ambayo nimebarikiwa nayo hadi sasa. Kama mvulana wa kijijini mwenye matamanio, sikuwahi kufikiria kuwa maisha yangenipeleka kwenye njia ya ajabu kama hii," Samidoh alisema kwenye Instagram.

Aliambatanisha taarifa yake na orodha ya Wakenya waliotunukiwa na kwa tuzo za rais mnamo Jumanne ambayo ilimuonyesha akiwa nambari 121.

"Kila hatua ya njia imekuwa ushuhuda wa nguvu ya ndoto, bidii na sapoti isiyo na shaka ya wapendwa wangu na ninyi, mashabiki wangu. Ninaamini kabisa kuwa mafanikio ni juhudi ya pamoja na ninashukuru daima kwa neema, upendo na msaada kutoka kwa Mungu na kutoka kwa watu wanaonizunguka," alisema.

Mwimbaji huyo pia alimshukuru rais William Ruto kwa kumtambua na akaahidi kuendelea kuweka juhudi zaidi katika tasnia hiyo.

“Asanteni nyote kwa upendo wenu usioyumba na msaada. Tuendelee kufanya mema huku tukiwatia moyo wengine njiani,” alisema.

Makumi ya mashabiki waliopata kuona chapisho la Samidoh walikusanyika chini yake wakiwa na maoni tofauti, shukrani na hata dhihaka.

Baadhi ya mashabiki hata walipendekeza kwamba seneta Karen Nyamu, ambaye ni mpenzi wa mwimbaji huyo alikuwa na jukumu la kutekeleza katika uteuzi wa wale waliotambuliwa.

“Karen anapata nini kama haki? Cz huyu bibi anakufanyia mambo mengi sana. Kama si yeye, sammy hungekuwa kiwango hiki. Mpe tu hatua sawa,” Hellennjokimwangi86 alisema.

Samidoh akajibu, “Hehe, si ningetafuta kwanza yake?”

Ririjoo_mso alitoa maoni, “Yani Karen hapati shukrani! Ama ni jiwe tu la kukanyaga katika safari yakoya kisiasa. ??”

Mwimbaji huyo akajibu, "Mwambie awithdraw atafute yake kwanza."

Jeymo_jim alitoa maoni: “Kijana cha assmio tuzo hizi zinakuwa hazina maana😂😂😂😂.

Akajibu, "Najua vile inakua aki."