Bahati na Diana Marua hatimaye watangaza ni lini watafanya harusi

Wapenzi hao walipaswa kufunga ndoa rasmi Desemba 12, 2023 lakini ilibidi waahirishe hafla hiyo.

Muhtasari

•Diana Marua wameapa kufanya harusi rasmi mwaka ujao wa 2024 baada ya mpango wao wa awali wa kufunga ndoa mwaka huu kuporomoka.

•Mwimbaji Bahati pia alithibitisha maneno ya mkewe kwa kusema "2024 NIMEAPA!!"

Diana Marua na Bahati
Image: INSTAGRAM// DIANA MARUA

Wanandoa mashuhuri Kelvin Bahati na Diana Marua wameapa kufanya harusi rasmi mwaka ujao wa 2024 baada ya mpango wao wa awali wa kufunga ndoa mwaka huu kuporomoka.

Siku ya Jumatatu asubuhi, Diana Marua alionyesha picha zake nzuri na mumewe wakifurahia matukio mazuri ya kimahaba wakati wa harusi ya rafiki yao waliyokuwa wamehudhuria takriban wiki moja iliyopita. Wawili hao walikuwa miongoni mwa wapambe wakati wa harusi ya Mkurugenzi Ritchie iliyofanyika wiki jana.

Katika sehemu ya maelezo ya picha hizo, mwanavlogu huyo wa video za YouTube mwenye wafuasi wengi alieleza hamu yake kubwa ya kufunga ndoa rasmi na Bahati, ambaye alimtambua kuwa rafiki yake bora.

“Siwezi kusubiri siku nitakayosema YES I DO kwa rafiki yangu bora @BahatiKenya.. Nakupenda mpenzi.. 2024 itakuwa mwaka wa The Bahatis,” Diana Marua aliandika na kuambatanisha taarifa hiyo kwa emoji ya pete.

Mwimbaji Bahati pia alithibitisha maneno ya mkewe kwa kusema "2024 NIMEAPA!!"

Wawili hao waliochumbiana rasmi mapema mwaka huu walikuwa wametangaza awali kwamba wangefunga harusi kubwa na nzuri mnamo Desemba 12, 2023. Harusi hiyo hata hivyo haikufanyika mnamo tarehe iliyotajwa lakini badala yake walihudhuria harusi ya rafiki yao Director Ritchie.

Huku wakimpongeza Director Ritchie na mkewe wiki iliyopita, wapenzi hao wawili walisema siku hiyo ilipaswa kuwa siku yao kubwa lakini kutokana na sababu zisizoweza kuepukika walilazimika kuighairi lakini wakaahidi kutoa tarehe mpya hivi karibuni.

"Leo ilitakiwa iwe siku ya harusi yetu lakini... Hongera sana marafiki zetu @Directorritchie na @RenaSolomon Tunayo furaha kuwa sehemu ya Line-Up yako tunapochukua maelezo ya jinsi tutakavyowaletea sherehe yetu kubwa. 💑 Tarehe Mpya za Harusi zitatangazwa hivi karibuni…” Bahati aliandika.

Takriban miezi miwili iliyopita, Bahati alifichua kuwa tayari amemtolea mahari mama huyo wa watoto wake watatu na akadokeza kuwa watafunga ndoa hivi karibuni.