Mke wa Steve Harvey avunja kimya kuhusu madai ya kumsaliti kimapenzi na mpishi, talaka

Marjorie alibainisha kuwa kila kitu kiko sawa nyumbani na akadai kwamba madai yanayoendelea ni upumbavu na ni ya uwongo.

Muhtasari

•Kumekuwa na uvumi mwingi kwamba wanandoa hao wako mbioni kutengana baada ya Steve kubaini kuwa mkewe amemsaliti kimapenzi.

•Kwa upande wake, Steve Harvey pia alipuuza uvumi huo na madai ya talaka akifafanua kuwa yeye na mkewe wako sawa.

Steve Harvey na mke wake Marjorie Harvey
Image: INSTAGRAM

Marjorie Harvey, mke wa mtangazaji maarufu wa televisheni Steve Harvey amevunja ukimya huku uvumi kwamba alitoka kimapenzi na mpishi na mlinzi wao ukiendelea.

Katika siku chache zilizopita, kumekuwa na uvumi mwingi kwamba wanandoa hao wako mbioni kutengana baada ya Steve kubaini kuwa mkewe amemsaliti kimapenzi.

Katika taarifa ya Jumatatu asubuhi hata hivyo, Marjorie alibainisha kuwa kila kitu kiko sawa nyumbani na akadokeza kwamba madai yote yanayoendelea ni upumbavu na ni ya uwongo.

Mama huyo wa watoto saba alichapisha blogu kuhusu ‘Jinsi ya kushughulikia kudanganywa’ na chini yake akawaomba watu waisome ili waelewe.

“Mimi na mume wangu huwa hatusimami kuzungumzia upumbavu na uwongo wote ambao umeenezwa kutuhusu. Hata hivyo ni anayepewa vingi, vingi huhitajika,” Marjorie aliandika kwenye mtandao wa Instagram.

Aliongeza, "Ninaelewa kuwa na jukwaa langu huja aina fulani ya jukumu kwa wale ambao wanaweza kutokuwa na nguvu kama sisi. Soma na ushiriki hii na wapendwa wako ambao labda hawajui jinsi ya kustahimili ipasavyo. Mungu Awabariki nyote.”

Pia alishiriki mstari wa Biblia kutoka katika 1 Petro 2;23 unaozungumzia njia bora ya kutenda mtu anaposhambuliwa na watu wengine.

“Walipomtupia matusi yao, hakulipiza kisasi; alipoteseka, hakutoa vitisho. Badala yake, alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki,” mstari wa Biblia unasema.

Kwa upande wake, Steve Harvey pia alipuuza uvumi huo na madai ya talaka akifafanua kuwa yeye na mkewe wako sawa.

Katika moja ya vipindi vyake vya runinga, mshereheshaji aliwataka watu wanaoeneza uvumi kutafuta kitu bora cha kufanya na kuacha kueneza habari za uwongo.

“Tunapata. Sijui mnafanya nini, lakini tafuta kitu kingine cha kufanya kwa sababu tuko sawa… Sina wakati wa uvumi na uvumi. Mungu amekuwa mwema kwangu, bado ninang'aa." Harvey alisema kwenye Invest Fest 2023.