Mkewe Guardian Angel, Esther Musila ajibu atahisi vipi iwapo mwanawe ataoa mke mzee

Esther Musila amemzidi umri mumewe Guardian Angel kwa takriban miongo miwili.

Muhtasari

•Musila alionekana kujibu kwa hasira na kutaka mwanamitandao huyo ajishughulishe na maisha yake mwenyewe.

•“Huyo atakuwa mwanangu ambaye atamleta na si wako, basi isikusumbue," Esther Musila alijibu kwa hasira.

Esther Musila
Image: INSTAGRAM

Mke wa mwimbaji wa nyimbo za injili Guardian Angel, Esther Musila alijibizana na mashabiki wake kwenye mtandao wa Tiktok ambao walionekana kumkosoa kuhusu ndoa yake.

Mwanamtandao mmoja alimuuliza swali kuhusu jinsi angefanya ikiwa mmoja wa wanawe ataoa mwanamke mwenye umri mkubwa kuliko yeye.

"Itakuwaje kama mwanao siku moja atakuletea mke ambaye ni mkubwa kuliko yeye utafeel aje?" mtumizi mmoja wa Tiktok alimuuliza.

Mama huyo wa watoto watatu wakubwa ambaye alionekana kutofurahishwa na swali hilo alionekana kujibu kwa hasira na kutaka mwanamitandao huyo ajishughulishe na maisha yake mwenyewe.

“Huyo atakuwa mwanangu ambaye atamleta na si wako, basi isikusumbue. Kuwa na wasiwasi kuhusu fedha zako, visigino vilivyopasuka, uhusiano, kuwa na shughuli nyingi,” Musila alijibu.

Shabiki mwingine pia alijikuta kwenye upande mbaya na mhasibu huyo mwenye umri wa miaka 53 baada ya kumshutumu kwa kumharibu Guardian Angel na kumtaka amshauri mwimbaji huyo mwenye umri wa miaka 35 kupata watoto kama yeye.

"Angalau mshauri Guardian kuwa na mtoto weeeuh unaharibu kijana wa wenyewe," shabiki aliandika.

Alijibu, ”Jishauri mwenyewe kwanza jinsi ya kuendesha maisha yako kabla ya kufikiria kuingilia maisha ya watu wengine. Maisha imekukalia ngumu na mdomo ndio kubwa.”

Tangu ajitose kwenye mahusiano na Guardian Angel takriban miaka mitatu iliyopita, Esther Musila ameshambuliwa mara nyingi kwenye mitandao ya kijamii mahusiano hayo, hoja kuu ikiwa tofauti kubwa kati ya umri wao.

Mama huyo wa watoto watatu amemzidi umri Guardian Angel kwa takriban miongo miwili, jambo ambalo linafikiriwa kuwa si la kawaida katika jamii nyingi. Walakini, wanandoa hao wanaonekana kuridhika na kufurahia ndoa yao ya mwaka mmoja na mara nyingi wamekuwa wakiwakosoa wakosoaji wao na kuwathibitisha kuwa wako sawa pamoja.

Mwaka jana, mwanamuziki Guardian Angel aliweka wazi kuwa kupata watoto sio kipaumbele katika ndoa yake na Esther Musila.

Katika mahojiano ya Juni, mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 32 alisema nguzo kuu uhusiano wao ni mapenzi na si watoto.

Guardian Angel alisema kwamba kupata mtoto na Bi Musila ni la ziada kutoka kwa Mungu  ambayo kwake si lazima wapate.

"Nilipoingia kwenye ndoa yetu, mtoto ni nambari mbili. Akija ama akose ni sawa. Nambari moja ni upendo wetu. Mungu akitaka kutupatia bonasi ya baraka ya mtoto ni sawa. Lakini kama haipo, hiyo ni bonasi, tunafurahia na tulicho nacho. Upendo wetu ndio ninaojali," Guardian alisema katika mahojiano na Plug TV.

Mwanamuziki huyo alisema upendo wao pekee umetosha na kueleza kuwa umemletea amani kubwa moyoni.

"Tukipata mtoto ni sawa, tukikosa pia haipunguzi chochote kwa upendo wangu kwa mke wangu," Alisema.

Wawili hao walifunga ndoa mnamo Januari 4 mwaka jana katika harusi ndogo iliyohudhuriwa na familia na marafiki wa karibu. Hii ilikuwa baada ya kuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi kwa zaidi ya mwaka mmoja.