Baada ya Kajala kumtenda, Harmonize amshukuru Mungu kwa kumpa mpenzi mpya!

Akimkaribisha maishani mwake, Harmonize alimsifia kidosho huyo na kumtaja kama wa kipekee anayeujua mchezo.

Muhtasari

• Harmonize alimvisha Kajala pete ya uchumba mwezi Juni mwaka jana lakini mapenzi yao yalibuma miezi sita baadae.

• Harmonize alitoa wimbo akiahidi kusalia bila mpenzi lakini ndio hivyo tena mapenzi ni kikohozi, keshanaswa tena!

Harmonize na mpenzi mpya,
Harmonize na mpenzi mpya,
Image: Instagram

Miezi kadhaa baada ya fununu kwamba Harmonize amebuma kwenye penzi na mwigizaji mkongwe Fridah Kajala, msanii huyo amepata mpenzi mpya.

Mwanadada mmoja ambaye ni mwanablogu wa mitandaoni, Sishikiki Sikamatiki, alipakia picha ya msanii huyo kwenye ukurasa wake na kumtakia kheri njema ya siku yake ya kuzaliwa.

Ikumbukwe Jumatano, msanii huyo wa Konde Gang alikuwa anasherehekea siku yake ya kuzaliwa, akidai kufikisha umri wa miaka 29.

Watu mbali mbali mitandaoni walipakia na kushiriki picha zake wakimtakia neema ya Mungu na afya tele anapoongeza mwaka mwingine.

Miongoni mwa hao ni mjasiriamali wa biashara za kuuza nguo, anayejiita Sishikiki Sikamatiki kwenye mtandao wa Instagram.

Mwanadada huyo ambaye hupiga mitikasi yake nchini Tanzania na Zambia alimwandikia Harmonize ujumbe murwa akimwambia kwamba anatumai sasa hayuko singo kwa sababu yeye yupo.

“Ningeandika aya lakini tayari unajua moyo unazungumza nini kwa ajili yako. ️ @harmonize_tz nadhani wewe sio #SINGLE tena najivunia hilo,” Sishikiki Sikamatiki aliandika.

 Harmonize kwa mbwembwe nyingi alimjibu kwamba hana wasiwasi tena kuhusu mapenzi kwani kwake tayari moyo wake umetuama.

Alimkaribisha kwenye himaya ya Konde Village akisema kwamba ni utendaji wa Mungu.

“Nakupenda 💕 ️ mwanamke tofauti mwenye upekee wa aina yake katika mchezo, karibu kwenye maisha yangu 😂 Mungu huyu,” Harmonize aliandika.

Harmonize baada ya kile kilitajwa kuwa ni kutendwa kimapenzi na Kajala, alionekana mwenye mashaka sana mpaka hakutaka kuweka wazi kilichotokea baina yake na Kajala hadi leo hii, ikiwa ni miezi Zaidi ya mitatu tangu fununu za kutengana kwao zivuje mitandaoni.

Msanii huyo alitimba studioni na kutoa wimbo akisema kwamba mapenzi kwake basi tena, wimbo alioupa jina ‘Single Again’ ambao unazidi kutamba kwenye chati za muziki, ikisemekana kwamba wimbo huo unashikilia kidedea katika mtandao wa Shazam nchini Zambia.

Kwa upande wake Kajala, pia hajawahi zungumzia wazi kilichojiri kwa mpenzi wake wa zamani ambaye wakati anamvisha pete ya uchumba mwezi Juni mwaka jana Milimani City, Kajala kwa madaha alikula yamini kwamba angempenda Harmonize jana, leo n ahata milele – ahadi ambayo hata hivyo imesalia kuwa historia na ndoto za alinacha.