Brian Chira ashikwe na afungwe kabisa, mimi siwezi mtoa seli - Eric Omondi

“Brian Chira ashikwe tu, iwe funzo kwa wengine. Watu wanatumia vibaya mitandao ya kijamii kuwatukana wengine na hajui kuna watu wamepata depression kwa sababu ya kudhihakiwa mitandaoni." - Omondi.

Muhtasari

• Chira alishikwa usiku wa Alhamisi katika kile kilisemekana kwamba alihatarisha maisha ya Azziad kwa kuanika namba yake mitandaoni.

Eric amtaka Chira kuomba Azziad msamaha.
Eric amtaka Chira kuomba Azziad msamaha.
Image: Instagram

Mchekeshaji ambaye ni mwanaharakati wa haki za binadamu Eric Omondi kwa mara ya kwanza amesema kwamba hatokwenda kumtoa TikToker Brian Chira seli baada ya kukamatwa na polisi usiku wa Alhamisi.

Chira alishikwa kwa kumchafulia TikToker mwenzake Azziad Nasenya jina na pia kuanika namba yake ya simu mitandaoni.

Omondi akizungumza na wanahabari wa mitandaoni, alisema kuwa yeye huwatoa maceleb wa kenya jela na kuwaokoa wale ambao wamejipata katika mkondo usio sahihi wa kisheria lakini kwa mara ya kwanza kwa Chira, hatoshiriki katika kumtoa ndani.

Omondi alisema kuwa TikToker huyo mwenye hulka ya kuwadhihaki watu mitandaoni ni sharti akae seli hadi apate adabu, akisema kuwa kitendo cha kuanika namba ya Nasenya si kizuri kwani ni kama kumweka katika hali ya hatari kwa usalama wake.

“Brian Chira ashikwe tu, iwe funzo kwa wengine. Watu wanatumia vibaya mitandao ya kijamii kuwatukana wengine na hajui kuna watu wamepata depression kwa sababu ya kudhihakiwa mitandaoni. Ashikwe afungwe mpaka apate adabu,” Omondi alisema.

“Simimi ndio huwatoa watu jela, huyo Chira aombe radhi ama afungwe. Mimi ndio hutoa watu jela lakini kwa mara ya kwanza hii ni mbaya siwezi. Uchukue simu ya mtu uweke mitandaoni, unamhatarisha. Unajua mtu anaweza tumia namba yako kukufuatilia, siendi kumtoa lakini pia sitaki afungwe, namwambia aombe msamaha,” Omondi aliongeza kwa kushauri.

Alimtaka Chira kuomba msamaha na akifanya hivyo atakwenda mwenyewe na kumtoa na hata kumfaulishia nauli ya kurudi Nakuru.

Chira alishikwa usiku wa Alhamisi katika kile kilisemekana kwamba alihatarisha maisha ya Azziad kwa kuanika namba yake mitandaoni lakini pia kumtamkia maneno yasiyoweza kuchapishika.

TikToker huyo amekuwa akionywa dhidi ya hulka hiyo mbaya ya kuwatukana watu pindi anapofungua TikTok yake na kufanya vipindi vya moja kwa moja haswa nyakati za usiku.

Wiki chache zilziopita, Oga Obinna alimshauri kutowajibu wanaomjia juu lakini ni kama hakusikia la mwadhini wala la mteka maji msikitini.