Pasta Ezekiel awaonya watu dhidi ya kusherehekea siku zao za kuzaliwa maarufu 'Birthdays'

“Usisherehekee siku yako ya kuzaliwa kama hujafanya jambo lolote la maana, subiri mpaka ufanye jambo la maana ndio usherehekee." Esekiel alisema.

Muhtasari

• Mchungaji huyo aliwapa changamoto waumini wa kanisa lake akiwauliza kama wamewahi msikia akisherehekea siku yake ya kuzaliwa.

Image: The star

Mchungaji wa kanisa la New Life Prayer Centre, Ezekiel Odero kwa mara nyingine tena amezua ukakasi mitandaoni baada ya video ya mahubiri yake tata kuhusu watu wanaosherehekea siku zao za kuzaliwa kuenezwa.

Katika video hiyo, mchungaji huyo mwenye mahubiri yanayochukuliwa kuwa yenye itikadi kali alionekana akiwakashifu na kuwaonya vikali waumini wake ambao wanapenda kusherehekea siku zao za kuzaliwa kila mwaka.

Pasta Ezekiel alihubiri akisema kwamba kusherehekea siku yako ya kuzaliwa si vibaya lakini pia haifai kuwa sherehe ya kila mtu bali yule tu ambaye amefanya kitu cha maana katika mwaka huo ndiye pekee anayestahili kusherehekea siku yake ya kuzaliwa.

“Usisherehekee siku yako ya kuzaliwa kama hujafanya jambo lolote la maana, subiri mpaka ufanye jambo la maana ndio usherehekee. Ndio maana tunasherehekea kufa na kufufuka kwa Yesu,” Ezekiel alisema.

Mchungaji huyo aliwapa changamoto waumini wa kanisa lake akiwauliza kama wamewahi msikia akisherehekea siku yake ya kuzaliwa.

Aliashiria kwamba mchungaji hafai kupata wakati au muda wa kwenda kusherehekea siku yake ya kuzaliwa, na kusema kwamba yeye hawezi jisherehekea bali wale watakaokuja baada yake ndio wataona kama watamsherehekea kulingana na matendo yake.

“Hakuna mwanajeshi anayesherehekea siku yake ya kuzaliwa, ukiwa msituni ni bunduki na risasi, unalaia sikio moja na lingine liko wazi. Mimi huwa najiuliza saa ngapi mtu anaenda kusherehekea siku yake ya kuzaliwa na yeye ni mchungaji na mapepo yanamsumbua?” aliuliza.