Gor Mahia yakatiza mkataba wa Dennis Oliech kwa kukosa nidhamu

oliech
oliech
Gor Mahia imekatiza mkataba na mshambulizi wake Dennis Oliech kutokana na visa vya utovu wa nidhamu.

Klabu hio inasema mchezo mbaya wa Oliech uwanjani na kukosekana kwake mazoezini mara kadha bila ya ruhusu ya klabu, ndio kumechangia kufurushwa kwake.

Klabu hio pia imemshtumu kwa kujitoa kuwania katika uchaguzi wa kisiasa, kinyume cha sheria za klabu. Oliech alitia saini mkataba wa miaka miwili na Kogallo mapema mwaka huu.

Arsenal ipo tayari kumruhusu mchezaji wa kimataifa wa Uhispania Nacho Monreal kujiunga na Real Sociedad wiki hii iwapo mchezaji huyo wa miaka 33 ataomba kuondoka.

Kwingineko mshambuliaji wa Chelsea Tammy Abraham anaelekea kupata mkataba mpya ambao huenda ukaongeza zaidi ya mara mbili malipo ya mchezaji huyo wa miaka 21 raia wa Uingereza ya pauni elfu 50 kwa wiki.

Barcelona wanaendelea na majaribio yao ya kumsajili tena Neymar kutoka PSG. Wawakilishi kutoka Barca akiwemo afisa mkuu Oscar Grau, walifanya mazungumzo ya kufana na meneja mkuu wa PSG Jean-Claude Blanc na mkurugenzi wa michezo Leonardo jijini Paris jana, lakini bado hawajakubaliana mkataba wowote.

Real Madrid pia wako katika kinyang'anyiro cha kumsajili Neymar kabla ya dirisha la uhamisho la Uhispania kufungwa Septemba tarehe 2.

Inter Milan bado wana matumaini ya kujadili mkataba wa mkopo na  Manchester United kwa ajili ya Alexis Sanchez. Mazungumzo kati ya klabu hizo mbili yanaendelea kwa ajili ya mkopo wa msimu ambao utaigharimu klabu hiyo ya Serie A chini ya pauni milioni 11.

Mchezaji huyo alijiunga na United kutoka Arsenal Januari mwaka wa 2018 kama sehemu ya mkataba wa kubadilishana na Henrikh Mkhitaryan lakini amefunga mabao 3 tu ya ligi ya Premier katika mechi 32 alizocheza.