Rekodi zilizovunjwa na Erling Haaland kufikia sasa

Halaand alivunja historia ya Ligi ya Mabingwa ya mchezaji aliyefikisha mabao 30kwa muda mfupi.

Muhtasari

•Haaland aliibuka kuwa mfungaji bora wa Manchester City katika msimu moja huku tayari akiwa na mabao 39 msimu huu. 

•Anashikilia rekodi ya kufunga mabao mengi zaidi kwenye Uwanja wa Etihad katika msimu mmoja wa Ligi Kuu.

Rekodi zilizovunjwa na Haaland kufikia sasa.
Image: ROSA MUMANYI

Usiku wa Jumanne, mshambulizi Erling Haaland alifunga mabao matano ya Manchester City wakati wa mechi ya mkondo wa pili ya kufuzu robo fainali ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya klabu ya RB Leipzig.

Mabao matano ya Halaand katika mechi ya Jumanne usiku yalimfanya kufikisha mabao 30 kwenye Ligi ya Mabingwa hivyo kumfanya kuwa mchezaji mwenye umri mdogo zaidi kuwahi kutinga hatua hiyo.

Pia alivunja historia ya Ligi ya Mabingwa kwa kuweka rekodi ya haraka zaidi ya kufunga mabao 30.

Mshambulizi huyo pia aliibuka kuwa mfungaji bora wa Manchester City katika msimu moja huku tayari akiwa na mabao 39 msimu huu. 

Mchezaji huyo wa Norway pia ameendelea kuweka rekodi kwenye Ligi Kuu. Kufikia sasa ameweza kufunga mabao 28 huku mechi 11  zikiwa bado hazijachezwa. 

Kwa sasa anashikilia rekodi ya kufunga mabao mengi zaidi kwenye Uwanja wa Etihad katika msimu mmoja wa Ligi Kuu.

Grafiki hii inaangazia rekodi ambazo ameweza kuweka kufikia sasa:-

  • Mfungaji bora wa Man City katika msimu mmoja (Mabao 39).
  • Aliyefikisha mabao 30 ya Ligi ya Mabingwa kwa muda mfupi. (Mechi 25)
  • Wa kwanza kufunga mabao 20 katika mkondo wa kwanza wa EPL.
  • Mwenye umri mdogo kufikisha mabao 30 katika Ligi ya Mabingwa.
  • Wa kwanza kufunga ‘hat-trick’ katika mechi 3 mfululizo za nyumbani za EPL.
  • Wa kwanza kufungia Man City kwenye mechi ya kwanza ya EPL Kuu na UCL.