Iran yawanyonga watu watatu kuhusiana na maandamano dhidi ya serikali

Waandamanaji wengine wanne wamenyongwa tangu mwezi Disemba.

Muhtasari

•Watatu hao walipatikana na hatia kwa madai yakuhusika katika shambulio la risasi lililowaua maafisa watatu wa usalama mjini Isfahan mwezi Novemba.

•Watatu ambao walinyongwa siku ya Ijumaa walikamatwa baada ya maandamano katika mji wa kati wa Isfahan mnamo 16 Novemba.

Image: BBC

Mamlaka nchini Iran imewanyonga wanaume watatu waliohukumiwa kifo kuhusiana na maandamano ya kupinga serikali mwaka jana, mahakama inasema.

Watatu hao walipatikana na hatia kwa madai yakuhusika katika shambulio la risasi lililowaua maafisa watatu wa usalama mjini Isfahan mwezi Novemba.

Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International linasema walikabiliwa na kesi zisizo za haki na wanadaiwa kuteswa.

Waandamanaji wengine wanne wamenyongwa tangu mwezi Disemba.

Makumi ya wengine wameripotiwa kuhukumiwa kifo au kushtakiwa kwa makosa ya mauaji.

Maandamano hayo yalienea katika Jamhuri hiyo ya Kiislamu kufuatia kifo cha Mahsa Amini, mwanamke wa Kikurdi mwenye umri wa miaka 22 ambaye alizuiliwa na polisi wa maadili mjini Tehran mwezi Septemba kwa madai ya kuvalia hijabu yake "isivyofaa".

Watatu ambao walinyongwa siku ya Ijumaa - Majid Kazemi, 30, Saleh Mirhashemi, 36, na Saeed Yaqoubi, 37 - walikamatwa baada ya maandamano katika mji wa kati wa Isfahan mnamo 16 Novemba.

Vyanzo vya habari viliiambia Amnesty International kwamba watu hao walikamatwa kwa nguvu, kisha kuteswa na kulazimishwa kutoa matamshi ya kuwatia hatiani ambayo yaliunda msingi wa kesi za jinai dhidi yao.