Rwanda yamkosoa rais wa DRC kwa kumfananisha Rais Kagame na Hitler

Ni ishara ya hivi punde ya uhusiano mbaya sana kati ya majirani hao.

Muhtasari

•Rwanda imemkosoa rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kwa kumfananisha rais wa Rwanda, Paul Kagame na Adolph Hitler.

•Katika mkutano wa kampeni za chaguzi Felix Tshisekedi alimshutumu rais wa Rwanda kwa kuwa na malengo ya kujitanua.

Image: BBC

Serikali ya Rwanda imemkosoa rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kwa kumfananisha rais wa Rwanda, Paul Kagame na Adolph Hitler.

Ni ishara ya hivi punde ya uhusiano mbaya sana kati ya majirani hao.

Nchi hizo mbili zimeshutumiana kila mmoja kwa kuunga mkono makundi ya waasi ili kuyumbisha nyingine.

Katika mkutano wa kampeni za chaguzi Felix Tshisekedi alimshutumu rais wa Rwanda kwa kuwa na malengo ya kujitanua.

Kwa muda mrefu amekuwa akiikosoa Rwanda kwa kupeleka jeshi lake ndani ya Congo.

Kisha akasema kama Paul Kagame angetaka kuwa kama Adolf Hitler ataishia kama yeye.

Msemaji wa serikali ya Rwanda alielezea maoni haya na uwepo wa waasi wa Kihutu wenye silaha mashariki mwa Congo kama vitisho vya wazi.

Serikali ya Kigali inakanusha lakini imekuwa ikishutumiwa vikali kwa kuunga mkono kundi la waasi la M23 linaloongozwa na Watutsi.

Limekuwa likiteka eneo la Congo na kulazimisha mamia ya maelfu ya watu kukimbia makazi yao.

Kuna hatari ya mzozo zaidi mashariki mwa Congo huku uhusiano kati ya majirani ukidorora zaidi.