Kijana wa kuranda mtaani ashangaza mahakama kwa lafudhi ya Kiingereza

Muhtasari

•Griffin Nyongesa alimwomba hakimu Jacqueline Ojwang asimpeleke jela kwa kosa ambalo alikuwa amelitenda.

• Jinsi alivyojieleza kwa lafudhi ya Uingereza ilishtua mahakama nzima kwani kawaida, familia nyingi za mitaani huchukuliwa kuwa hazisomi. 

Griffin Nyongesa akiwa mahakamani
Griffin Nyongesa akiwa mahakamani
Image: CLAUSE MASIKA

Kijana wa kuranda mtaani anayekusanya taka katika eneo la Westlands na viunga vyake Jumatatu alishangaza mahakama ya Kibera kwa lafudhi yake ya Uingereza alipopanda kizimbani kujitetea. 

Griffin Nyongesa alimwomba hakimu Jacqueline Ojwang asimpeleke jela kwa kosa ambalo alikuwa amelitenda.

Alizungumza baada ya kukiri kosa la kuwa na roli 24 za bangi zenye thamani ya Sh1,200. 

Kulingana na shtaka, Nyongesa alitenda kosa hilo mnamo Juni 9 kando ya barabara ya Chiromo huko Westlands ndani ya Kaunti ya Nairobi. 

Mwendesha mashtaka Brenda Maiyo aliambia mahakama kuwa mshtakiwa alikamatwa baada ya maafisa waliokuwa kwenye doria ya kawaida kuwa na shaka naye. 

Walimkamata na kumpata akiwa na  roli za bangi zenye thamani ya Sh1,200. 

Katika kujitetea kwake, jamaa huyo ambaye alionekana kuwa na elimu nzuri alisema kuwa yeye ni mtu wa familia na alikuwa na Sh 1,000 tu kati yake na umaskini. 

“Kama unavyoniona hapa mheshimiwa, nina Sh1,000 pekee kati yangu na umasikini, tafadhali nisamehe,” aliambia hakimu.

 Jinsi alivyojieleza kwa lafudhi ya Uingereza ilishtua mahakama nzima kwani kawaida, familia nyingi za mitaani huchukuliwa kuwa hazisomi. 

Nyongesa aliambia mahakama kuwa amekuwa akiishi mitaani kwa zaidi ya miaka 16 na amekuwa akivuta bangi huku akiokota taka.  

"Mimi huvuta bangi ili niweze kukusanya takataka bila mafadhaiko," alisema.

 Hakimu aliagiza kesi hiyo litajwe tena Juni 22 na kuamuru ripoti ya uangalizi iwasilishwe mahakamani.