Nairobi: Mwanamke Mchina afikishwa mahakamani kwa kuiba korodani za mbuzi

Mwanamke huyo raia wa Uchina alishtakiwa kwa kuiba korodani za beberu zenye thamani ya milioni 6 na kuzisafirisha kwao kutoka Kenya.

Muhtasari

• Aliiomba mahakama kumuachilia kwa dhamana akisema ni mjamzito.

• Kesi hiyo itasikilizwa tena Aprili 5.

Korodani za beberu.
Korodani za beberu.
Image: Mpasho

Mwanamke mmoja Raia wa Uchina Jumatano alifikishwa katika mahakama ya Nairobi kwa kuiba na kusafirisha nje korodani za mbuzi.

Kwa mujibu wa nyaraka za mahakama, Bi Lei Yunyan anadaiwa kujipatia korodani hizo zenye thamani ya Shilingi milioni sita kwa njia ya udanganyifu, jarida moja liliripoti.

Mwanamke huyo aliyetambulika kwa jina Yunyan alisemekana kushiriki katika upataji wa korodani hizo kati ya Septemba mwaka 2021 na Novemba 2022 alisafirisha korodani za beberu kutoka Kenya kwenda nje zipatazo Zaidi ya kilo 804.

Marsa Goto Ado, mlalamishi katika kesi hiyo alisema aliwasilisha korodani za mbuzi kilo 804 na kilo zingine 113 kwa kampuni inayodaiwa kuendeshwa na Mchina huyo lakini hakulipwa pesa zake kiasi cha milioni 6 na ushee.

Bi Yunyan alikana mashtaka na akaachiliwa kwa dhamana ya Sh500,000 pesa taslimu au bondi mbadala ya Shilingi milioni moja na Hakimu Mkuu Mwandamizi.

Alitakiwa kuwasilisha pasipoti yake ya usafiri mahakamani akisubiri kesi yake kutajwa tena, kwani awali kulikuwa na wasiwasi wa kumnyima bondi kwa kile upande wa mlalamishi ulisema huenda angetoroka nchini.

Kesi hiyo itatajwa tena Aprili 5.