Mwanamke ashtakiwa kwa kutumia jina la Raila kumlaghai mwekezaji wa Nigeria Ksh 25m

Mahakama iliambiwa kwamba raia huyo wa Nigeria asingetumbukia katika ulaghai huo kama si kutajiwa jina la mtu anayedaiwa kuwa na uhusiano wa kifamilia na Bwana Raila Odinga.

Mahakama ya Milimani mjini Nairobi
Mahakama ya Milimani mjini Nairobi

Mwanamke mmoja Mkenya amefikishwa mahakamani kwa tuhuma za kutumia jina la kinara wa upinzani Raila Odinga na kumlaghai mwekezaji wa Nigeria kima cha shilingi milioni 25.

Kwa mujibu wa ripoti ya Nation, mwanamke huyo alipokea pesa hizo kutoka kwa mfanyibiashara wa Nigeria kwa lengo la kufadhili usambazaji wa vyandarua vya kujikinga dhidi ya malaria kwenda kwa taasisi ya Kemsa.

Ripoti hiyo inasema kwamba mwanamke huyo alitumia ujanja wa kumhadaa mwekezaji huyo kwamba kandarasi ya kusambaza vyandarua hivyo ilikuwa ya mkaza mwana wa Odinga ambaye kwa kipindi hicho alikuwa ameishiwa na pesa na alikuwa na uhitaji wa ufadhili ili kukamilisha kandarasi yake ya usambazaji wa vyandarua.

Alidaiwa kumdanganya raia huyo wa kigeni kwamba baada ya kumpa ksh 25m, angepata faida baada ya kandaras hiyo kukamilika.

Mahakama iliambiwa kwamba raia huyo wa Nigeria asingetumbukia katika ulaghai huo kama si kutajiwa jina la mtu anayedaiwa kuwa na uhusiano wa kifamilia na Bwana Raila Odinga.

Mwanamke huyo anadaiwa kupokea pesa hizo kwa viwango tofauti kati ya Juni na Desemba mwaka 2022 jijini Nairobi.

Hata hivyo, mshtakiwa huyo alikanusha mashtaka yote ya ulaghai dhidi yake na kutaka kuachiliwa kwa dhamana, jambo ambalo lilipingwa vikali na upande wa mashtaka.