logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mombasa: Raia wa Kigeni wakamatwa wakitunuku watu PhDs baada ya mafunzo ya siku 3

Washukiwa hao wanne ni pamoja na Wakenya 2, Mmarekani mmoja na Mpakistani mmoja ambao walikuwa wanatoa mafunzo ya siku 3 hotelini kisha kuwatunuku PhD na Masters.

image
na MOSES SAGWEjournalist

Mahakama14 February 2025 - 08:58

Muhtasari


  • Washukiwa hao wanne ni pamoja na Wakenya 2, Mmarekani mmoja na Mpakistani mmoja ambao walikuwa wanatoa mafunzo ya siku 3 hotelini kisha kuwatunuku PhD na Masters.

pingu

MAKACHERO kutoka katika idara ya upelelezi wa jinai, DCI wamewakamata washukiwa ambao wamekuwa wakiwazawadi wakenya katika kaunti ya Mombasa shahada za uzamili na uzamivu baada ya mafunzo ya siku tatu tu.

Katika taarifa iliyochapishwa kwenye akaunti yao ya X mnamo Februari 13, 2025, DCI ilifichua kwamba watu hao walikuwa wakiendesha shughuli zao katika chuo kikuu cha muda kilichoanzishwa katika Kaunti ya Mombasa.

Washukiwa hao wanne ni pamoja na Wakenya 2, Mmarekani mmoja na Mpakistani mmoja ambao walikuwa wanatoa mafunzo ya siku 3 kwa watu katika hoteli moja kisha kuwatunuku PhD na Masters.

“Raia wawili wa kigeni ni miongoni mwa washukiwa wanne ambao wametiwa mbaroni katika oparesheni kali inayolenga chuo kikuu cha simu ambacho kilikuwa kimepewa makao kwa muda katika hoteli moja kaunti ya Mombasa. Wanne hao walipatikana wakitoa Shahada za Uzamili na Uzamivu kwa washiriki waliochangamka waliokuwa wamepata mafunzo kwa siku tatu pekee,” DCI ilitaarifu.

Wanne hao walikamatwa na maafisa wa kutekeleza sheria kutoka Kituo cha Polisi cha Bamburi, baada ya kupata taarifa kuhusu shughuli za kutisha za kundi hilo.

Baadhi ya shahada zilizotunukiwa kwa njia ya udanganyifu ni pamoja na Shahada tatu za Uzamili ya Utawala wa Biashara (Uongozi na Menejimenti) na Shahada za Uzamivu mbili za Uongozi.

Watuhumiwa hao wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Sheria ya Shanzu ambapo walisomewa shitaka la Kutoa Shahada Bila Ithibati ya Vyuo Vikuu vya Nje Kinyume na Kifungu cha 28(2) kikisomwa na kifungu cha 5 cha Sheria ya Vyuo Vikuu, DCI iliarifu.

Washtakiwa hao walikana hatia ambapo walipewa dhamana ya Ksh 400,000 na mdhamini sawa na lazima wafanyike kwa kiapo mbele ya mahakama ya wajibu au dhamana ya pesa taslimu ya Ksh 300,000.

Pasipoti za wageni hao wawili pia ziliwekwa mahakamani na kutajwa kupangwa tarehe 18 Februari, 2025.

“DCI inaonya kuwa hakuna juhudi zitasalia katika kuwakamata washukiwa wanaotoa vyeti kwa njia ya ulaghai kwa watu ambao wanashindwa kutoa jasho,” ripoti ilisema.

Mnamo Aprili 2024, Rais William Ruto alifichua kuwa zaidi ya watu 2,100 walio na vyeti ghushi vya masomo walikuwa wakifanyia kazi serikali.

Wakati huo, Ruto aliamuru walio na vyeti vya ulaghai kuacha nyadhifa za serikali na kutafuta kulipwa pesa walizochuma kimakosa kutoka kwa serikali.

“Sasa tutakabiliana na janga la ufisadi moja kwa moja, iwe ni katika kaunti, iwe katika serikali ya kitaifa. Hebu fikiria, ukaguzi rahisi wa watu wanaofanya kazi serikalini umefichua kuwa tuna watu 2,100 walio na vyeti ghushi (vya kitaaluma) wanaofanya kazi serikalini,” Ruto alisema.

 

 

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved