Jomo Kenyatta: Mfahamu mwanawe Uhuru ambaye nyumba yake ilivamiwa na polisi

Jomo anaonekana kurithi mielekeo ya kisiasa na amekuwa akifuata nyayo za babake Uhuru.

Muhtasari

•Uhuru  alifoka kwa ghadhabu baada ya polisi kudaiwa kuvamia nyumba ya mwanawe Jomo katika mtaa wa Karen, Nairobi.

•Jomo yuko kwenye ndoa na Fiona Achola na kwa pamoja wana watoto wawili, Wanjiru na Uhuru.

Mtoto wa Rais Uhuru Kenyatta Jomo Kenyatta akiwa na mkewe Fiona Achola.
Mtoto wa Rais Uhuru Kenyatta Jomo Kenyatta akiwa na mkewe Fiona Achola.
Image: HISANI

Siku ya Ijumaa, rais mstaafu Uhuru Kenyatta alifoka kwa ghadhabu baada ya polisi kudaiwa kuvamia nyumba ya mwanawe Jomo katika mtaa wa Karen, Nairobi.

Hii ilimfanya rais huyo wa nne wa Jamhuri ya Kenya kuvunja ukimya wake wa muda mrefu kuhusu kile ambacho kimekuwa kikiendelea nchini.

Rais huyo wa zamani alikosoa serikali kwa kumfuata mama yake na watoto wake.

Alimwomba Rais William Ruto badala yake akabiliane naye ana kwa ana na kuacha familia yake.

Uhuru alisema kuwa alilinda nchi alipokuwa rais wa nne lakini sasa atailinda familia yake.

Lakini mtoto wa Uhuru, Jomo Kenyatta ni nani?

Rais huyo wa zamani ana watoto watatu wanaojulikana kama Jomo, Jaba na Ngina Kenyatta.

Jomo ndiye mtoto mkubwa kati ya ndugu watatu na alizaliwa Aprili 1989.

Yeye ni mhitimu wa Chuo cha Hilton na Micheal House katika KwaZulu Natal Midlands, Afrika Kusini.

Yuko kwenye ndoa na Fiona Achola na kwa pamoja wana watoto wawili, Wanjiru na Uhuru.

Watoto wao wawili walipewa majina ya Uhuru na aliyekuwa First lady Margaret.

Achola anadaiwa kutoka katika ukoo wa kiongozi wa kisiasa wa Waluo Dkt William Odongo Omamo.

Jomo ameweka maisha yake binafsi nje ya vyombo vya habari. Licha ya hayo, mara nyingi amekuwa akionekana katika matukio yaliyosimamiwa na baba yake, wakati akiwa mkuu wa nchi.

Jomo anaonekana kurithi mielekeo ya kisiasa na amekuwa akifuata nyayo za babake Uhuru.