Elon Musk apoteza taji la mtu tajiri zaidi duniani kwa Jeff Bezos

Musk sasa ana utajiri wa dola bilioni 197.7 huku utajiri wa Bezos ukiwa dola bilioni 200.3.

Muhtasari

•Musk amepoteza nafasi yake katika kipimo cha Mabilionea cha Bloomberg kwa Jeff Bezos baada ya hisa katika kampuni ya Tesla kushuka kwa 7.2% Jumatatu.

Image: BBC

Kwa mara ya kwanza baada ya zaidi ya miezi tisa, Elon Musk amevuliwa taji la kuwa mtu tajiri zaidi duniani.

Musk amepoteza nafasi yake katika kipimo cha Mabilionea cha Bloomberg kwa Jeff Bezos baada ya hisa katika kampuni ya Tesla kushuka kwa 7.2% Jumatatu.

Musk sasa ana utajiri wa dola bilioni 197.7 huku utajiri wa Bezos ukiwa dola bilioni 200.3.

Ni mara ya kwanza kwa Bezos, 60, mwanzilishi wa kampuni ya Amazon kushika nafasi ya kwanza ya Bloomberg ya watu tajiri zaidi tangu 2021.

Pengo la utajiri kati ya Musk, 52, na Bezos, ambalo wakati mmoja lilikuwa kubwa kama dola bilioni 142, limekuwa likipungua huku hisa za Amazon na Tesla zikienda pande tofauti.

Ingawa kampuni zote mbili ni kati ya zenye hisa zinazojulikana sana ambazo zimekuza masoko ya hisa ya Marekani, hisa za Amazon zimeongezeka zaidi ya mara mbili tangu mwishoni mwa 2022 na ziko katika rekodi ya juu.

Kampuni ya Tesla iko chini karibu 50% kutoka kilele chake cha 2021.

Hisa za kampuni ya Tesla zilishuka Jumatatu baada ya data ya awali kuonyesha usafirishaji kutoka kwa kiwanda chake huko Shanghai ulipungua hadi chini zaidi katika kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja.

Wakati huo huo, kampuni ya Amazon, imekuwa na ukuaji bora wa mauzo mtandaoni tangu mwanzoni mwa janga la corona.