Matatu yenye uwezo wa kubeba abiria 14 yakamatwa ikiwa imerundika wanafunzi 31

Kulingana na NTSA, dereva wa matatu alifanikiwa kutoroka kukamatwa akiwaacha wanafunzi kwenye matatu hiyo.

Muhtasari

• Haya yanajiri huku kukiwa na juhudi mpya za serikali kudhibiti visa vinavyoongezeka vya ajali za barabarani zinazoendelea kupoteza maisha.

Ajali
Ajali
Image: HISANI

Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi na Usalama (NTSA) imeikamata matatu ya abiria 14 ambayo ilipatikana ikiwa na wanafunzi 31 kutoka Kaunti ya Tharaka Nithi.

Kulingana na NTSA, dereva wa matatu alifanikiwa kutoroka kukamatwa akiwaacha wanafunzi kwenye matatu hiyo.

Gari hilo lilizuiliwa Meru kwa hatua zaidi.

“Madereva na wasimamizi wa shule waliokabidhiwa usalama wa watoto wetu lazima waelewe wajibu wao,” ilisema NTSA.

Haya yanajiri huku kukiwa na juhudi mpya za serikali kudhibiti visa vinavyoongezeka vya ajali za barabarani zinazoendelea kupoteza maisha.

Wiki iliyopita, Waziri wa Uchukuzi Kipchumba Murkomen alitangaza hatua mpya za kukabiliana na ongezeko la ajali za barabarani, ikiwa ni pamoja na agizo la kurejea kwa maafisa wa NTSA barabarani.

Murkomen alitangaza kuwa NTSA itaanza mara moja kutekeleza kanuni za usalama barabarani kwa ushirikiano na Huduma ya Kitaifa ya Polisi, na kubatilisha agizo la 2018 la aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta lililowaondolea mamlaka hiyo jukumu hilo.

Waziri huyo aliagiza NTSA na polisi kuzidisha juhudi za utekelezaji barabarani kote nchini na kukamata magari yasiyofaa kuwa barabarani ambayo hayana ushirikiano na mfumo wa usimamizi wa usalama barabarani kwa ajili ya kusambaza data za kidhibiti mwendo.

Pia aliagiza kuhakikiwa mara moja kwa madereva wanaoendesha Magari ya Watumishi wa Umma (PSV) na magari makubwa ya kibiashara.