'Hakuna atakaye lala njaa,' Ruto awaambia waathiriwa wa mafuriko

Mathare ilikuwa mojawapo ya maeneo yaliyoathiriwa kwa kiasi kikubwa na mafuriko huko Nairobi.

Muhtasari
  • Rais alizuru eneo la Kiamaiko ambapo alihutubia wenyeji akiwahakikishia uungwaji mkono wa serikali.
Rais Ruto kuongeza idadi ya watoza ushuru kwenye masoko, mitaa.
Rais Ruto kuongeza idadi ya watoza ushuru kwenye masoko, mitaa.
Image: Facebook

Rais William Ruto amewahakikishia waathiriwa wa mafuriko huko Mathare kwamba utawala wake utawaunga mkono.

Akizungumza Jumatatu alipofanya ziara ya ghafla, Rais alisema serikali imejitolea kuhakikisha kuwa kila familia iliyoathiriwa ina chakula cha kutosha.

Alisema serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuwapatia chakula.

"Serikali itasimama nawe. Hakuna mwananchi atalala njaa, hakuna mtoto atalala njaa. Tumeweka pesa ya kutosha ya kununua chakula cha kila mtu ameathirika hapa nairobi na Kenya mzima..." Ruto alisema.

Rais alizuru eneo la Kiamaiko ambapo alihutubia wenyeji akiwahakikishia uungwaji mkono wa serikali.

Alisema serikali itaipa kila familia iliyoathiriwa Sh10,000 ili kuwasaidia kutafuta makazi mbadala kwa muda wa miezi mitatu huku serikali ikitafuta suluhu la kudumu.

Mathare ilikuwa mojawapo ya maeneo yaliyoathiriwa kwa kiasi kikubwa na mafuriko huko Nairobi.

Ruto alisema utawala wake utawashughulikia wote walioathirika hadi watakapokuwa na uwezo wa kujihudumia wenyewe.

Idadi ya waliofariki kutokana na mafuriko kufikia Jumapili ilifikia 228.

Msemaji wa serikali Isaac Mwaura alisema mafuriko yanayoendelea pia yameacha watu 164 na majeraha huku wengine 72 wakiripotiwa kutoweka.

Katika taarifa yake Jumapili, Mwaura alisema takriban watu 212,630 kutoka kaya 42,526 wamelazimika kuyahama makazi yao.

Kwa jumla, alisema, watu 223,198 wameathiriwa na mafuriko nchini kote.

Mwaura alisema Kaunti za Homa Bay, Kajiado, Nakuru, Mandera na Nairobi ndizo zilizoathiriwa zaidi na mvua kubwa inayoendelea kunyesha ambayo imesababisha mafuriko kwa idadi ambayo haijawahi kushuhudiwa.