Rais Ruto atazamia kushiriki biashara na Korea Kusini

Kenya itajiunga na South Korea katika kung’amua nafasi zinazotokana na uvumbuzi wa teknolojia

Muhtasari

•Kwa mujibu wa ikulu, ziara hii inaipa Kenya nafasi murua ya kuzungumza  kuhusu ushirikiano wa mikataba ya kibiashara na nchi ya South Korea.

•Rais atakuwa anazuru nchi Korea Kusini kwa awamu ya pili baada ya kuzuru huko mnamo Novemba mwaka wa 2022.

RAIS WILLIAM RUTO
Image: TWITTER

Rais William Ruto anatarajiwa kutua mjini Seoul, South Korea mnamo Jumatatu jioni ili kuungana na viongozi wengine katika kuzuru mkutano wa kilele baina ya Korea na Afrika na viongozi kadhaa. Rais  anatazamia kujadiliana na wenyeji, South Korea kuhusu mikataba ya biashara.

Ziara hii ndiyo ya kwanza kuwahi kufanyika baina ya Korea na Afrika. Vilevile, Seoul ndio mji mkuu wa hivi punde wa kualika viongozi wa Afrika katika mkutano huo wa kilele. Baadhi ya viongozi hamsini na wanne wa Afrika walianza kuwasili mjini Seoul mnamo Jumamosi.

Viongozi waliothibitisha kuwasili mumo kutoka kanda ya Afrika mashariki ni pamoja na rais Samia Suluhu wa Tanzania pamoja na Paul Kagame wa Rwanda. Rais Yoweri Museveni wa Uganda atawakilishwa na makamu wake Jessica Alupo.

Kwa mujibu wa ikulu, ziara hii inaipa Kenya nafasi murua ya kuzungumza  kuhusu ushirikiano wa mikataba ya kibiashara na nchi ya South Korea ili kusaidia katika kustawisha biashara na uwekezaji.

"Ziara hii vilevile itaipa Kenya na Korea Kusini fursa ya kuanzisha mazungumzo  ya ushirikiano baina ya nchi hizo mbili,” ikulu ilisema.

Rais atakuwa anazuru nchi Korea Kusini kwa awamu ya pili baada ya kuzuru huko mnamo Novemba mwaka wa 2022.

Katika siku za nyuma, Rais Ruto aliwasihi wabunge wa nchi hiyo kukubali hatua ambayo itarahisisha shughuli za kibiashara miongoni mwa Kenya na South Korea ikiwemo na mataifa mengine ya Afrika.

“Usawa wa kibiashara unawaletea neema Korea na bunge na itakuwa kipaumbele katika kusuluhisha hali hii,” alisema rais Ruto baada ya kuzungumza na wabunge wan chi hiyo.

“Kenya itajiunga na South Korea katika kung’amua nafasi zinazotokana na uvumbuzi wa teknolojia ikiwemo ukuaji wa viwanda vya kondakta nusu, Kenya vilevile itajiunga na taasisi ya kimataifa ya chanjo ili kukuza ukuaji wa chanjo zao.” Alisema rais.

Naam, ziara hii inakusudiwa kuleta manufaa kwa wananchi wa Kenya na pia barani Afrika.