Charlene Ruto awatembelea wanauguza majeraha hospitalini kutokana na machafuko ya maandamano

“Naamini ni wakati wa kutafakari na kuponya kama taifa tunapotafuta misimamo yetu ya ndani kabisa ya uzalendo, msamaha na kuunganishwa kama watu wamoja! Mungu ibariki Kenya! SISI NI KITU KIMOJA!” aliomba.

Muhtasari

• Binti huyo wa rais pia alisema ni muda sasa kwa watu wote kuketi chini na kupiga tathmini na kusameheana kama taifa

Charlene Ruto
Charlene Ruto
Image: Facebook

Binti wa kwanza wa taifa, Charlene Ruto katika siku za hivi karibuni amekuwa akijishughulisha na shughuli kadhaa nchini.

Moja ya shughuli hizo imempeleka katika hsoptalini ambapo alikwenda kuwatembelea baadhi ya vijana waliopata majeraha wakati wa makabiliano kwenye maandamano ya kupinga mswada wa fedha wa mwaka 2024.

Binti Ruto kupitia ukurasa wake wa X alichapisha picha na video akiwa kwenye wadi za vijana hao waliojitokeza wakiwa wazima kushiriki maandamano na mwisho wa siku kujikuta na majeraha ya risasi kwenye vitanda vya hospitali mbalimbali, wengi wao wakilazwa katika hospitali kuu ya Kenyatta.

Binti Ruto aliwasikitikia vijana hao na kusema kwamba ni tukio ambalo halingestahili kutokea.

“Ilikuwa ni siku ya hisia sana kuwatembelea baadhi ya vijana na wananchi waliojipata kuwa wahanga wa bahati mbaya wa machafuko yaliyojitokeza katika siku za hivi karibuni,” Binti Ruto aliandika.

Charlene ambaye pia ni mshirika katika mashirika ya uchangiaji damu nchini aliyashukuru baadhi ya mashirika hayo na Wakenya kwa kujitokeza kwa wingi kuchangia damu kwa ajili ya wenzao waliopata majeraha wakati wa maandamano ya Gen Z kupinga kupitishwa kwa mswada.

“Ningependa kushukuru  @official_ktta, idara ya madaktari wakiwemo MedicsforKE, @kenyanbybloodfoundation, mabalozi wenzangu wa damu na timu nyingine nyingi kwa kuchangia damu inayohitajika katika kipindi hiki,” alisema.

Binti huyo wa rais pia alisema ni muda sasa kwa watu wote kuketi chini na kupiga tathmini na kusameheana kama taifa.

“Naamini ni wakati wa kutafakari na kuponya kama taifa tunapotafuta misimamo yetu ya ndani kabisa ya uzalendo, msamaha na kuunganishwa kama watu wamoja! Mungu ibariki Kenya! SISI NI KITU KIMOJA!” aliomba.

Maandamano hayo ya Amani yaligeuka na kuwa vurugu katika wiki yake ya pili baada ya kile kilichotajwa kuwa ni makundi ya vijana wenye nia mbaya kuingilia maandamano ya GenZ.

Katika machafuko hayo, mashirika ya kutetea haki za binadamu yamedai kuwa vifo vilikuwa zaidi ya 40 huku serikali ikisema ni watu chini ya 25 tu waliofariki.