Binamu 2 wafumaniwa wakishiriki mapenzi, watiwa voboko na kupitishwa kwa moto

Wawili hao wote wa miaka 40 kwenda mbele walichapwa viboko na kulazimishwa kupita kwa tanuru la moto wa nyasi kama njia ya kuwatakasa.

Muhtasari

• Kulingana na tamaduni ya jamii hiyo, watu wa nasaba wanaopatikana wakishiriki mapenzi wanachapwa na kufanyiwa tambiko la kupita kwenye moto.

• Kisha majivu ya moto huo hutupwa kwenye mto ulioko karibu kama njia moja ya kutokomeza laana hiyo.

Binamu wafumaniwa wakishiriki mapenzi wachapwa viboko kuondoa laana.
Binamu wafumaniwa wakishiriki mapenzi wachapwa viboko kuondoa laana.
Image: BBC NEWS

Binamu wawili walicharazwa viboko hadharani mbele ya watu baada ya kufumaniwa wakishiriki mapenzi.

Kulingana na jarida moja la Uganda, binamu hao wawili msichana na mvulana walitiwa viboko vikali hadharani kama njia moja ya kutokomeza mwiko huo unaoenda kinyume na tamaduni za jamii nyingi za Kiafrika.

Wawili hao kutoka Wilaya ya Kumi, wote wakiwa na umri wa miaka arobaini kwenda juu, walichapwa viboko na wakazi wa kijiji cha Oogoria baada ya "kukamatwa" katika msako wa usiku Jumamosi iliyopita, jarida hilo liliripoti.

Walipatikana katika nyumba ya mwanamume huyo kufuatia uangalizi wa wiki mbili baada ya kushukiwa kuwa walikuwa wakijihusisha na mapenzi. Ukoo wao unakataza ngono kati ya jamaa.

Wanakijiji walisema walikamatwa saa nane asubuhi wakiwa katika tukio hilo.

Wakuu wa koo zao baada ya hapo walifanya sherehe ya utakaso ambapo mwanamume na mwanamke walipokea viboko kadhaa vya mijeledi. Kisha wakalipa faini ya mbuzi ili watekelezaji wawe na karamu ya "kuosha aibu waliyoipata kwa kuona uchi wao wakati wa kukamatwa kwao", ripoti hiyo ilisimulia.

Wawili hao kisha walilazimishwa kuingia kwenye tanuru la nyasi ambalo lilichomwa moto. Kisha waliruhusiwa kutoroka tanuru huku wasimamizi wa koo wakiwapiga.

Kulingana na wazee wa ukoo huo, wawili ambao hupatikana wakishiriki mapenzi wakiwa kutoka nasaba moja ya damu, hucharazwa viboko na kulazimishwa kupita kwenye tanuru la moto wanyasi.

Wawili hao hulazimika kutoroka huku wakipigwa viboko na kila mmoja anafaa kutoroka kwenda njia yake. Endapo watakimbia kwenda njia sawa, inaashiria kwamba hawajatubu dhambi zao na hulazimishwa kurudia mchakato wa kupita kwenye tanuru hilo.

Baada ya kumalizika kwa mchakato huo, majivu ambayo husalia hutupwa kwenye mto ulioko karibu, jarida lilinukuu maelezo ya mila ya jamii hiyo.