MSWADA TATA WA FEDHA

Wanaounga mkono mswada wa fedha, hawaupundi ila wanataka kumfurahisha Rais - Fatuma Abdi

Mnaunga mkono ili kumfurahisha Rais, pia nanyi mnaumia ni vile hamsemi

Muhtasari

•Najua baadhi ya wabunge hata hawaungi mswada huu mkono kwa kupenda, wanafanya hivyo ili kutii amri ya Rais.

•Wiki chache zilizopita, Rais alitoa vitisho kwa wabunge kuhusiana na mswada tata wa fedha 2023, ambapo alisema angetaka kumwona mbunge yeyote atakayeupinga mswada huo wakati utawasilishwa bungeni.

Mwakilishi wa kike wa Wajir Fatuma Abdi. Picha: STEPHEN ASARIKO
Mwakilishi wa kike wa Wajir Fatuma Abdi. Picha: STEPHEN ASARIKO

Mswada tata wa fedha mwaka wa 2023 umewakilishwa bungeni kwa mara nyingine kusomwa na kuwaruhusu wabunge watoe mchango wao kuuhusu. Baadhi ya wabunge wameunga mkono huku wengine wakipinga.

Mwakilishi wa Kike kaunti ya Wajir amekiri kwamba wabunge wa muungano tawala wa Kenya Kwanza wanaounga mkono mswada huo, si kwa kupenda kwao ila ni kutaka kutii amri ya ya Rais Ruto.

Fatuma, alieleza kwamba, Wakenya wengi nchini kwa sasa wanaonesha kutoridhika na pendekezo la mswada huo, hasa ukiangazia kiwango cha ushuru hasa katika bidhaa muhimu za matumizi ya kila siku.

“Najua baadhi ya wabunge hata hawaungi mswada huu mkono kwa kupenda, wanafanya hivyo ili kutii amri ya Rais.” Alisema katika bunge.

Wiki chache zilizopita, Rais alitoa vitisho kwa wabunge kuhusiana na mswada tata wa fedha 2023, ambapo alisema angetaka kumwona mbunge yeyote atakayeupinga mswada huo wakati utawasilishwa bungeni.

Mswada huo ambao umeibua hisia mseto miongoni mwa raia, huku wabunge wakitoa maoni yao Wakenya wangali wanasubiri kujua hatma yao katika upande wa hali ngumu ya maisha.

Wabunge wengi waliopinga ushuru wa nyumba za bei nafuu, ambalo ni pendekezo katika kipengele cha mswada huo, wanauliza nyumba zinazokadiriwa kujengwa zitafaidi vipi zaidi ya Wakenya milioni tano, iwapo zinajengwa nyumba 50,000.

Haya janajiri huku Wakenya wakilalamikia hali ngumu ya maisha, huku wakiomba kunusuriwa na wabunge wao kutokana na mswada huo wa fedha unaolenga kuongezeka kwa ushuru.