Maafisa wa GSU wachukua usukani nyumbani kwa Ruto Sugoi na shambani

Usalama nyumbani kwa Ruto Sugoi umeimarishwa zaidi huku maafisa zaidi ya 50 wa GSU wakiwasili

Muhtasari

•Maafisa wengine wa GSU pia wamechukua ulinzi katika makazi ya Ruto mjini Eldoret na shamba lake karibu na Eldoret.

•Wakazi wa Eldoret wamekuwa wakisherehekea tangu Ruto kutangazwa kuwa rais mteule.

Maafisa wa GSU wakiwa nyumbani kwa Rais Mteule William Ruto Sugoi huko Uasin Gishu.
Maafisa wa GSU wakiwa nyumbani kwa Rais Mteule William Ruto Sugoi huko Uasin Gishu.
Image: MATHEWS NDANYI

Usalama katika nyumba ya Rais mteule William Ruto Sugoi umeimarishwa zaidi huku maafisa zaidi ya 50 wa GSU wakiwasili mle.

Maafisa wengine wa GSU pia wamechukua ulinzi katika makazi ya Ruto mjini Eldoret na shamba lake karibu na Eldoret.

Maafisa wa AP waliokuwa wakilinda nyumba ya Sugoi hawakuonekana wakati wanahabari walipotembea pale Jumatano.

Maafisa wa GSU katika lango kuu la kuingilia waliwazuia wanahabari hao kupiga picha langoni, tofauti na hali ya utulivu ilivyokuwa siku mbili zilizopita.

"Lazima utafute kibali kinachohitajika ikiwa nyinyi ni waandishi wa habari na mnataka kupiga picha au video," afisa mmoja alisema.

Usalama umeimarishwa hatua kwa hatua tangu Ruto atangazwe kuwa Rais mteule na IEBC siku ya Jumatatu.

Timu zingine za usalama zilionekana zikishika doria katika barabara karibu na nyumba ya Sugoi, takriban kilomita 30 kutoka Eldoret kutoka kwa barabara kuu kuelekea Webuye.

Kamanda wa polisi kaunti ya Uasin Gishu Ayub Gitonga alisema usalama ulisalia kuwa mkali katika eneo hilo huku biashara zikiendelea baada ya uchaguzi mkuu wa Agosti 9 na kutangazwa kwa matokeo.

Ombi la kupinga matokeo linalotarajiwa kuwasilishwa katika Mahakama ya Juu linaweza kuleta mvutano, haswa baada ya uamuzi wa mahakama kuthibitisha au kubatilisha kuchaguliwa kwa Ruto. Ikiwa ushindi wa Ruto hautathibitishwa, basi Raila Odinga wa Azimio atakuwa ameshinda kesi.

“Tunawahakikishia wakazi wa kaunti yetu kwamba usalama wao umetunzwa vyema huku wakiendelea na shughuli za kawaida,” Gitonga alisema.

Wakazi wamekuwa wakisherehekea tangu Ruto kutangazwa kuwa rais mteule.

Viongozi wa UDA katika eneo hilo, hata hivyo, walifutilia mbali msafara wa sherehe uliokuwa ufanyike kutoka Kapenguria huko Pokot Magharibi kupitia Kitale, Iten mjini, Eldoret na kisha Kapsabet.

Viongozi wote waliochaguliwa katika eneo hili wakiongozwa na Seneta Mteule wa UDA wa Uasin Gishu Jackson Mandago na magavana, miongoni mwa wengine, walipaswa kuongoza msafara huo.

“Tuna furaha kwa Rais mteule na tutakuwa na shughuli za kumshukuru Mungu,” Mandago alisema.

Vyanzo vya habari vilisema msafara huo ulisimamishwa ili kusubiri matokeo ya ombi la Mahakama ya Juu linalotarajiwa kuwasilishwa na timu ya Azimo.

Kinara wa Azimio Raila Odinga amekataa matokeo ya uchaguzi na uamuzi wa mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati kumtangaza Ruto kuwa rais mteule.

Mandago ni miongoni mwa viongozi katika eneo hilo ambao wamempongeza Ruto. Wengine ni magavana wa UDA Stephen Sang wa Nandi, Wesley Rotich wa Elgeyo Marakwet na Simon Kachapin wa Pokot Magharibi.

UDA ilishinda takriban viti vyote vya uchaguzi katika eneo hilo, ambalo ni ngome ya kisiasa ya Ruto.

Mratibu wa chama hicho katika eneo hilo Paul Kiprop alisema wanajivunia wakazi kwa kutii wito wa kuwapigia kura wagombeaji wa UDA.

Mratibu wa chama hicho katika eneo hilo Paul Kiprop alisema wanajivunia wakazi kwa kutii wito wa kuwapigia kura wagombeaji wa UDA.

"Tumefanya vyema na tutakuwa na uongozi thabiti kuanzia mabunge yetu hadi ngazi ya kitaifa," Kiprop alisema.

Alisema itakuwa rahisi kwa chama kutekeleza sera na mipango yake ya maendeleo kwa sababu ya kutawala katika mabunge na Bunge.