MCK kufanya mkutano na wadau kuwadhibiti waandishi wa habari feki

Omwoyo alidokeza kuwa tume hiyo inafanya kazi ndani ya mipaka ya sheria kama ilivyoainishwa katika kifungu cha 6(d) cha Sheria

Muhtasari
  • Mkurugenzi Mtendaji Omwoyo alisema zaidi kwamba tume inaendelea kujitolea kukuza mazingira ambayo yanafaa kwa wataalamu
Mkurugenzi mkuu wa MCK, David Omwoyo
Image: MCK (Facebook)

Baraza la Vyombo vya Habari Kenya (MCK) litakutana na wawakilishi kutoka sekta ya vyombo vya habari mnamo Ijumaa, Januari 27, ili kuanzisha mfumo wa kukuza taaluma ya uandishi wa habari.

Mkurugenzi Mtendaji wa MCK David Omwoyo amesema katika taarifa yake siku ya Alhamisi kwamba ongezeko la watu wanaojifanya wanahabari na kutumia vyeo vyao vya uongo kuwahadaa wananchi ndilo lililochochea mkutano huo.

“Imefika kwetu kwamba kuna ongezeko la walaghai wanaojifanya wanahabari na watendaji wa vyombo vya habari ambao hupata matukio kwa nia ya kulaghai na kuwanyanyasa watu,” alisema Omwoyo.

“Kuhusiana na hili, Baraza la Vyombo vya Habari nchini Kenya limepanga mkutano na washikadau wa tasnia hii Ijumaa, 27. Januari 2023, ili kutoa jukwaa la kujadili suala hilo na kukubaliana kuhusu hatua za kivitendo za kuimarisha taaluma na kushughulikia kesi zinazoibuka za walaghai wanaojifanya waandishi wa habari."

Mkurugenzi Mtendaji Omwoyo alisema zaidi kwamba tume inaendelea kujitolea kukuza mazingira ambayo yanafaa kwa wataalamu wa vyombo vya habari na wanahabari "kushughulikia masuala muhimu yanayoathiri sekta hiyo."

“MCK itasalia msitari wa mbele katika kulinda uaminifu wa vyombo vya habari na wanahabari kwa kuhakikisha kuwa wanahabari walioidhinishwa pekee ndio wanaruhusiwa kufanya kazi nchini, kulingana na vipengee vyetu vya Kikatiba,” alibainisha Omwoyo.

Omwoyo alidokeza kuwa tume hiyo inafanya kazi ndani ya mipaka ya sheria kama ilivyoainishwa katika kifungu cha 6(d) cha Sheria ya Baraza la Vyombo vya Habari, 2013, ambayo inaruhusu ukuzaji na uboreshaji wa viwango vya maadili na taaluma miongoni mwa wanahabari na mashirika ya habari.