Raila astaafu kama mwakilishi mkuu wa AUC, Moussa Faki atangaza

Muda wa kuhudumu wa Raila kama Mwakilishi Mkuu wa Umoja wa Afrika kwa Maendeleo ya Miundombinu umefikia kikomo.

Muhtasari

• Faki alimpongeza Raila kwa kukubali jukumu hilo akisema kwamba amekuwa nguzo katika uboreshaji wa miundomsingi kama kipaumbele kikuu barani.

KINARA WA AZIMIO RAILA ODINGA
Image: ANDREW KASUKU

Muda wa kuhudumu wa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga kama Mwakilishi Mkuu wa Umoja wa Afrika kwa Maendeleo ya Miundombinu umefikia kikomo.

Kukamilika kwa hatamu ya Raila kulitangazwa na Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika Moussa Faki Mahamat.

Katika barua yake iliyoandikwa Februari 19, Faki alimpongeza kiongozi huyo mkuu wa zamani kwa kukubali jukumu hilo, akiongeza kuwa uongozi wa Raila umekuwa nguzo katika uboreshaji wa miundomsingi kama kipaumbele kikuu barani.

Raila alishikilia wadhifa huo huku Shirika la NEPAD likijiandaa kuchukua udhibiti kamili wa idara hiyo.

"Mabadiliko ya Shirika la NEPAD kuwa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Afrika sasa yamekamilika, na lina mamlaka kamili ya kutekeleza ajenda ya Bara la Afrika kuhusu miundombinu," Faki alisema.

"Jukumu lako katika safari hii, Mheshimiwa, limekuwa la thamani sana. Niruhusu nitoe shukrani zangu za dhati kwa kukubali kuhudumu katika wadjifa huu wakati wa kipindi cha mpito, ambacho sasa kimefikia hitimisho la furaha."

Raila aliteuliwa kuwa Mwakilishi Mkuu wa Maendeleo ya Miundombinu barani Afrika mwezi Oktoba 2018.

"Uamuzi huu ni sehemu ya harakati za Umoja wa Afrika kuharakisha ujumuishaji wa bara hili kupitia miundombinu, ili kukuza ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu," Faki alisema.

"Pia atasaidia AUC na mipango ya NEPAD kuhimiza kuongezwa kwa misaada kutoka kwa washirika wa maendeleo kupiga jeki mikakati ya miundombinu barani Afrika."