Mvulana wa kidato cha 3 akamatwa kwa kumchoma kisu mtahiniwa wa KCSE

Makundi yanayopigana yalikuwa yamejazana shuleni na kuanza kupigana kabla ya polisi kuitwa.

Muhtasari
  • Mkurugenzi wa elimu kaunti ya Lamu Joshua Kaaga alisema shule hiyo huenda ikafunguliwa wiki ijayo.
Pingu
Image: Radio Jambo

Polisi wa Lamu wamemkamata kijana wa miaka 17 ambaye alimdunga kisu mwanafunzi mwenzake katika shule yao huko Lamu Mashariki mnamo Jumatatu.

Mshukiwa, Mohamed Idarus, alitolewa nje ya nyumba aliyokuwa amejificha katika kijiji cha Tchundwa Jumatano jioni.

Kamanda wa polisi kaunti ya Lamu William Samoei alithibitisha kuwa mshukiwa huyo anazuiliwa katika kituo cha polisi cha Kizingitini ambapo anahojiwa kufuatia shambulizi hilo.

Mshukiwa huyo alikuwa amekimbia muda mfupi baada ya kumchoma kisu mwanafunzi wa kidato cha nne Mohamed Bakari.

Kisa hicho kilitokea saa za asubuhi huku walioshuhudia wakisema mshambuliaji alichomoa kisu ambacho alikuwa amekiweka chini ya shati lake na kwenda kumchoma marehemu mara kadhaa.

Marehemu alimwaga damu muda mfupi baada ya hapo huku mshukiwa akisemekana kukimbia.

Shule hiyo imefungwa kwa muda usiojulikana na wanafunzi kurudishwa nyumbani kufuatia machafuko yaliyotokea kufuatia kisa hicho.

Marehemu alizikwa siku hiyo hiyo siku ya Jumatatu katika makaburi ya Faza Town kwa mujibu wa mila za Kiislamu chini ya ulinzi mkali.

Kamishna huyo wa kaunti alisema mshukiwa huyo sasa anakabiliwa na mashtaka ya mauaji na atafikishwa mahakamani wakati wowote kuanzia sasa.

“Tumemkamata mtuhumiwa na tunamshikilia katika kituo cha polisi cha Kizingitini anakohojiwa. Tunakusudia kufikishwa mahakamani hivi karibuni,” alisema Samoei.

Mvutano bado unaendelea kati ya kijiji cha Faza ambako marehemu anatoka na kijiji cha mvamizi cha Tchundwa huko Lamu Mashariki.

Makundi yanayopigana yalikuwa yamejazana shuleni na kuanza kupigana kabla ya polisi kuitwa.

Jamii inaomba haki itendeke kwa marehemu.

Mkurugenzi wa elimu kaunti ya Lamu Joshua Kaaga alisema shule hiyo huenda ikafunguliwa wiki ijayo.