Mwanaume amuua mkewe kwa mshale Baringo

Polisi waliweza kupata mshale ambao unadaiwa kutumika katika mauaji.

Muhtasari

•Silas Barjipa anaripotiwa kutekeleza mauaji hayo mnamo Jumatatu usiku katika eneo la Kibonjos, Baringo ya Kati.

•Baadhi ya wakazi ambao walishuhudia walisema wanandoa hao walikuwa wakizozana kabla ya mauaji hayo kutokea. 

CRIME
Image: MAKTABA

Polisi katika kaunti ya Baringo wanamzuilia mwanaume mmoja kwa madai ya kumuua mkewe kufuatia mzozo wa kinyumbani.

Silas Barjipa anaripotiwa kutekeleza mauaji hayo mnamo Jumatatu usiku katika eneo la Kibonjos, Baringo ya Kati.

Naibu Kamishna wa Kaunti Ndogo ya Baringo ya Kati, Reuben Ratemo alithibitisha tukio hilo na kusema kuwa wanafanya uchunguzi.

"Ni kweli kwamba mwanamke aliripotiwa kuuawa na mumewe. Ingawa bado hatujabaini ukweli wote, wakaazi wanasema mshukiwa alikuwa amelewa na alikuwa akizozana na mkewe usiku huo,” alisema.

Ratemo alisema wanashuku mshukiwa alimchoma mkewe kwa mshale na kubainisha kwamba polisi waliweza kupata silaha hiyo inayodaiwa kutumika katika mauaji. 

Alisema mshukiwa atafikishwa mahakamani endapo atapatikana na hatia baada ya uchunguzi kukamilika.

Baadhi ya wakazi ambao walishuhudia walisema wanandoa hao walikuwa wakizozana kabla ya mauaji hayo kutokea.

Mshukiwa sasa anazuiliwa katika kituo cha polisi cha Kabarnet huku mwili wa mkewe ukiwa umehifadhiwa katika chumba cha maiti cha Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Baringo.