Azimio-Kenya Kwanza wakubaliana kuhusu mabadiliko ya IEBC

Alisema kamati ya mazungumzo imeweza kupiga hatua zitakazoongoza mchakato wa mazungumzo katika siku 59 zijazo.

Muhtasari
  • Mbunge huyo wa Kikuyu aliongeza kuwa jopo la IEBC litakuwa miongoni mwa washikadau walioalikwa wakati kamati hiyo itakapoanza mazungumzo na washikadau.
KINARA WA WIPER KALONZO MUSYOKA NA KIONGOZI WA WENGI KATIKA SENETI KIMANI ICHUNG'WAH WAKIWA BOMAS WAKATI WA MAZUNGUMZO YA PANDE MBILI 30/AGOSTI/2023
Image: TWITTER

Muungano wa Kenya Kwanza na Azimio la Umoja umekubali kuruhusu Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka kuendelea na majukumu yake.

Wakizungumza Bomas Jumatano, Timu hiyo inayoongozwa na aliyekuwa Makamu wa Rais Kalonzo Musyoka na Mbunge wa Kikuyu Kimani Ichung'wah ilisema kuwa jukumu la jopo hilo halitaingiliwa.

Hata hivyo, Ichung'wah alisema kuwa kufanya hivyo hakuzuii kamati hiyo kujadili masuala yanayohusu IEBC, na hivyo basi, wameandikia jopo ilani ya mahakama, kuwaarifu kuhusu kutendeka kwa kamati hiyo.

“Kwa hiyo hata wanapoendelea na kazi zao, wanatambua kuwa ni sehemu ya masuala tunayojishughulisha nayo,” alisema.

Mbunge huyo wa Kikuyu aliongeza kuwa jopo la IEBC litakuwa miongoni mwa washikadau walioalikwa wakati kamati hiyo itakapoanza mazungumzo na washikadau.

Kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka alisema jopo la IEBC ambalo jukumu lake ni kuajiri mwenyekiti na Makamishna sita wa IEBC wanaweza kusikia kutoka kwa kamati ya mazungumzo.

Alisema kamati ya mazungumzo imeweza kupiga hatua zitakazoongoza mchakato wa mazungumzo katika siku 59 zijazo.

“Uaminifu, uwazi na uadilifu ndio msingi wa mazungumzo ya kweli na hilo ndilo tunalokuza hapa Bomas of Kenya na Viongozi wenzetu wa Kamati ya Kitaifa ya Mazungumzo wakishirikiana na Ichung’wah,” Musyoka alisema.

Rais William Ruto mwezi Februari aliteua jopo la uteuzi wa wanachama saba.

Ruto aliwachagua Bethuel Sugut, Novence Euralia Atieno, Charity S. Kisotu, Evans Misati James, Benson Ngugi Njeri, Nelson Makanda (Mwenyekiti) na Fatuma Saman kuongoza zoezi hilo.

Hii ilikuwa baada ya kutia saini Mswada wa IEBC (Marekebisho) wa 2022 kuwa sheria inayoweka mazingira ya kuundwa kwa jopo la uteuzi wa wanachama saba kuwaajiri makamishna wapya.