Cristiano Ronaldo aonekana uwanjani Real Madrid - kunani?

Ronaldo amekuwa akitumia uwanja wa mazoezi wa Real Madrid kujiweka sawa.

Muhtasari

•Baada ya mkataba wake na Manchester United kufutwa mwezi uliopita, Ronaldo yuko huru kujiunga na klabu nyingine Januari 1.

•Ronaldo alifanya mazoezi peke yake katika kambi ya Real ya Valdebebas na hakuna chaguo la kurejea katika klabu hiyo ya Uhispania.

Image: BBC

Cristiano Ronaldo amekuwa akitumia uwanja wa mazoezi wa Real Madrid kujiweka sawa baada ya Ureno kutolewa kwenye Kombe la Dunia.

Baada ya mkataba wake na Manchester United kufutwa mwezi uliopita, Ronaldo yuko huru kujiunga na klabu nyingine Januari 1.

Klabu ya Saudi Arabia Al-Nassr imetoa ofa ya pesa nyingi kwa mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 37, ingawa inafahamika kuwa ana machaguo mingine.

Ronaldo alifanya mazoezi peke yake katika kambi ya Real ya Valdebebas na hakuna chaguo la kurejea katika klabu hiyo ya Uhispania.

Muda wa pili wa Ronaldo katika klabu ya Manchester United ulifikia kikomo baada ya mahojiano yenye utata ambapo mshindi huyo mara tano wa tuzo ya Ballon d'Or aliikosoa klabu hiyo na kusema "hana heshima" kwa meneja Erik ten Hag.

Hayo yalijiri siku mbili kabla ya Ureno kuanza kampeni ya Kombe la Dunia na Ronaldo kuanza michezo yao mitatu ya kwanza, akijibu kwa hasira alipotolewa katika mchezo wa mwisho wa kundi dhidi ya Korea Kusini.

Shirikisho la Soka la Ureno lilikanusha kuwa Ronaldo alitishia kuondoka kwenye kikosi hicho baada ya kuambiwa hataanza mchezo wa hatua ya 16 bora dhidi ya Uswizi, na badala yake Goncalo Ramos alifunga mabao mengi katika ushindi wa mabao 6-1.

Michuano hiyo nchini Qatar ilitarajiwa kuwa nafasi ya mwisho kwa Ronaldo kushinda Kombe la Dunia, na aliingia akitokea benchi dhidi ya Uswizi na Morocco lakini hakuweza kuizuia timu hiyo ya Afrika kuwatoa Ureno.