Crystal Palace yamrejesha Roy Hodgson kutoka kustaafu baada ya kumtimua Viera

Hodgson atahudumu kama meneja wa Palace hadi mwishoni mwa msimu.

Muhtasari

•Palace walitangaza kwamba mkufunzi huyo mwenye umri wa miaka 75 atachukua usukani kwa kipindi cha msimu kilichasalia.

•Mwezi Mei 2021 alitangaza kwamba angejiuzulu mwishoni mwa msimu wa EPL 2020/21.

Roy Hodgson
Image: HISANI

Crystal Palace wamemrejesha meneja wao wa zamani Roy Hodgson ili kujaza viatu vya Patrice Viera ambaye kandarasi yake na klabu hiyo ilikatizwa wiki iliyopita.

Katika taarifa yao ya Jumanne, Palace walitangaza kwamba mkufunzi huyo mwenye umri wa miaka 75 atachukua usukani kwa kipindi cha msimu kilichasalia.

"Roy Hodgson ameteuliwa kuwa meneja wa Crystal Palace hadi mwisho wa msimu. Paddy McCarthy atachukua nafasi ya meneja msaidizi wake, na Ray Lewington anarejea kama kocha wa kikosi cha kwanza," taarifa ya klabu hiyo ilisema.

"Dean Kiely ataendelea kuwa mkufunzi wa walinda lango. Karibu teba, Roy,"

Hodgson alisema ni tukio la heshima kurejea katika klabu hiyo kipenzi chake tangu utotoni na akaeleza nia yake ya kuisaidia kushinda mechi.

"Crystal Palace inajulikana kwa ari yake ya kupigana, na sina shaka kwamba wafuasi wetu wote watapigana nasi, kuanzia na mechi ya Leicester City wiki moja ijayo Jumamosi."

Palace ilimpiga karamu meneja Patrice Viera mnamo Machi 17, kufuatia msururu wa matokeo hafifu kwenye Ligi Kuu.

Roy Hodgson aliteuliwa kwa mara ya kwanza kama meneja wa Crystal Palace mwaka wa 2017 na alihudumu katika wadhifa huo hadi Mei 2021 alipotangaza kwamba angejiuzulu mwishoni mwa msimu wa EPL 2020/21.

"Kwa kweli ninaondoka kwenye soka kwa muda, lakini nani anajua siku zijazo itakuwaje? Ni wakati ambao huwezi kusema haiwezikani.Nimeona watu wengi wakistaafu huku mbwembwe zikiwa zimepamba moto, wakaibuka tena mahali fulani kwa muda mfupi sana. Ningependelea kutofanya hivyo," alisema.

Mnamo Januari 25, 2022, kocha huyo wa Uingereza alirejea Premier League alipoteuliwa kuwa meneja wa Watford.