AFCON 2027: CAF yakamilisha ukaguzi wa miundombinu Kenya, Tanzania na Uganda

Mataifa yote matatu yameagizwa kutekeleza kwa pamoja maelekezo yaliyotolewa ili kufikia lengo la Afrika Mashariki kuandaa mashindano hayo.

Muhtasari

•Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania Wallace Karia amezishukuru Serikali za nchi hizo kwa ushirikiano waliotoa kufanikisha ukaguzi.

•Rais Karia ametoa rai kwa mataifa yote matatu kutekeleza kwa pamoja maelekezo yaliyotolewa ili kufikia lengo la Afrika Mashariki kuandaa mashindano hayo

Image: BBC

Timu ya Wakaguzi wa utayari wa nchi za Tanzania, Kenya na Uganda kuwa wenyeji AFCON 2027, kutoka Shirikisho la Mpira Afrika (CAF) imehitimisha ukaguzi wao salama Agosti 2, 2023 Zanzibar kwa kikao cha majumuisho kilichoongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni,Sanaa na Michezo wa Tanzania Saidi Yakubu.

Akizungumza mara baada ya kikao hicho, Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania Wallace Karia amezishukuru Serikali za nchi hizo kwa ushirikiano waliotoa kufanikisha ukaguzi huo ikiwemo nia ya kuomba kuwa wenyeji wa mashindano hayo.

“Ukaguzi umemalizika vizuri, kwa kweli wameona tupo ‘serious’ na kuna mambo ambayo wametuelekeza tuyafanye, kwa upande wetu kama Tanzania bara na Zanzibar yapo mengi yamefanyika kwa sababu wakandarasi wapo site na vitu vinaonekana, wameelekeza hili jambo hili tulifanye kwa pamoja na wametoa siku 10 ili kukamilisha nyaraka zote zinazohitajika kulingana na maelekezo yao,” amesema Rais Karia.

Aidha, Rais Karia ametoa rai kwa mataifa yote matatu kutekeleza kwa pamoja maelekezo yaliyotolewa ili kufikia lengo la Afrika Mashariki kuandaa mashindano hayo ambayo hayajawahi kufanyika katika ukanda huo na nchi hizo zinatakiwa kukamilisha miundombinu ya michezo itakayotumika kwenye mashindano hayo kabla ya Desemba 2025.