'Mzee' Ronaldo ajionea fahari kuwapiku vijana wadogo kama Haaland katika ufungaji mabao

Ronaldo aliibuka mchezaji mwenye mabao mengi kwa mwaka 2023 mzima akiwapiku vijana wachanga kama Harry Kane wa Bayern, Haaland wa Man City, Mbappe wa PSG miongoni mwa wengine.

Muhtasari

• "Nilikuwa mfungaji bora zaidi msimu huu nikiwa na karibu miaka 39… fikiria kuwapiga wanyama wachanga kama Haaland, najionea fahari!".

• Ronaldo, ambaye sasa ana umri wa miaka 39, amefunga mabao 20 katika mechi 18 za SPL msimu huu,

Haaland na Ronaldo.
Haaland na Ronaldo.
Image: Facebook

Mchezaji wa Ureno na AL Nassr, Christiano Ronaldo amejionea fahari kubwa kuendelea kuvunja rekodi miaka nenda miaka rudi hata wakati wengi wanaona kama umri wake umekwenda sana kucheza soka.

Mchezaji huyo akizungumza katika hafla ya kupeanwa kwa tuzo za Globe Soccer mjini Dubai, alisema kwamba hivi karibuni anaingia miaka 39 lakini bado yuko katika viwango bora Zaidi kuwazidi vijana wadogo wenye nguvu katika soka.

Mchezaji huyo alijimiminia sifa kwa kuibuka mchezaji nambari moja kwa ufungaji mabao mwaka 2023 mbele ya magwiji kama Erling Haaland wa Manchester City, Harry Kane wa Bayern Munich na hata Kylian Mbappe wa PSG.

"Nilikuwa mfungaji bora zaidi msimu huu nikiwa na karibu miaka 39… fikiria kuwapiga wanyama wachanga kama Haaland, najionea fahari!".

Ronaldo, ambaye sasa ana umri wa miaka 39, amefunga mabao 20 katika mechi 18 za SPL msimu huu, na Al Nassr wanashika nafasi ya pili kwenye jedwali, pointi saba nyuma ya Al Hilal, wanaojivunia Neymar, Aleksandar Mitrovic na Ruben Neves miongoni mwa safu zao.

Ronaldo alisisitiza imani yake kwamba ligi ya Saudia inaweza kuwa moja ya mgawanyiko unaoongoza duniani, na kwamba alifurahishwa na uamuzi ambao alichukua kuanzisha athari za wachezaji wenye majina makubwa wanaowasili Saudi Arabia.

"Ninaamini watakuwa katika [ligi] tatu au nne bora duniani na, hatua kwa hatua, tutafikia hilo," Ronaldo alisema.

"Nilidhani [Saudi Arabia] ingekuwa hatua nzuri kwangu. Kwa nini nisipe nafasi kwa nchi nyingine, kwa soka langu na shauku yangu, kubadili fikra? Kwa nini isiwe hivyo? Nina uwezo wa kufanya hivyo. Sina kiburi; Nilisema hivyo mwaka mmoja uliopita.

“Mambo yanabadilika; dunia inabadilika, soka inabadilika, sheria zinabadilika. Kila kitu hubadilika.

“Hatua yangu ilikuwa nzuri. Najisikia furaha sana; wachezaji wengi, makocha, wakurugenzi, hata wataalamu wa lishe wanahamia huko. Wasaudi wako katika harakati hizo. Itachukua [muda mrefu], lakini katika maisha, tunasema, hatua kwa hatua, [kufikia] kiwango cha juu zaidi.”