Rodri, kiungo wa Man City afichua kwa nini Arsenal ilishindwa katika mbio za ubingwa wa EPL

"Arsenal walikuwa na msimu wa kushangaza, lakini nadhani tofauti ilikuwa ukomavu wa akili. Wakati walikuja kucheza nasi pale Etihad, niliwaona nikasema, ‘Ah, hawa jamaa hawataki kutushinda, wanataka sare tu."

Muhtasari

• City wamemaliza wakiwa na pointi 91 huku Arsenal, wakiwa na pointi 89, walilazimika kukaa nafasi ya pili kwa msimu wa pili mfululizo licha ya kushinda 2-1 nyumbani dhidi ya Everton.

Rodri akisherehekea bao.
Rodri akisherehekea bao.
Image: Premier League

Rodri, kiungo wa kati wa Manchester City amefichua jinsi walifanikiwa kuipiku Arsenal katika mbio za ubingwa wa ligi kuu ya premia, EPL msimu huu ambao umekamilika wikendi iliyopita.

Kwa muda mrefu, Arsenal walikuwa wameongoza katika msimamo wa jedwali la ligi hiyo baada ya Liverpool kuteleza na kuonekana kujiondoa katika mbio za ubingwa.

Arsenal waliongoza huku Man City ikiwa nyuma yao unyo unyo lakini mwisho wa yote, City ikaibuka washindi kwa kuiacha Arsenal kwa pointi mbili kileleni mwa jedwali.

Rodri alifunga City ikiilaza West Ham United 3-1 huko Etihad Jumapili na kushinda taji hilo pointi mbili mbele ya Arsenal, ambao waliwakimbiza hadi siku ya mwisho ya msimu wa kusisimua.

City wamemaliza wakiwa na pointi 91 huku Arsenal, wakiwa na pointi 89, walilazimika kukaa nafasi ya pili kwa msimu wa pili mfululizo licha ya kushinda 2-1 nyumbani dhidi ya Everton.

Alipoulizwa ni nini kilileta tofauti hiyo, Rodri aliiambia Optus Sport kuwa ilitokana na mawazo ya timu hizo mbili.

"Arsenal pia wanastahili (sifa), walikuwa na msimu wa kushangaza, lakini nadhani tofauti ilikuwa hapa," Mhispania huyo alisema akionyesha kichwa chake.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 aliangazia safu ya ulinzi ya Arsenal kwenye uwanja wa Etihad mwishoni mwa mwezi Machi ambayo iliisha kwa sare tasa huku mabingwa City wakishindwa kufunga bao licha ya kutawala kwa kumiliki mpira kwa asilimia 72.

“Wakati Arsenal walikuja kucheza nasi pale Etihad, niliwaona nikasema, ‘Ah, hawa jamaa hawataki kutushinda, wanataka sare tu’ na mawazo hayo, sidhani kama tungefanya kwa njia hiyo.”

"Na tuliwakamata (katika mbio za ubingwa). Mwishoni, ukitupa pointi moja, tutashinda mechi saba, nane za mwisho ingawa ni ngumu sana. Kwa hivyo nadhani hiyo inaonyesha mawazo yetu."

City wana nafasi ya kushinda taji lingine msimu huu watakapomenyana na Manchester United katika fainali ya Kombe la FA wikendi ijayo. "Pia ni muhimu sana kwetu kufanya mara mbili," Rodri aliongeza.